Afrika Mashariki yaomboleza kifo cha hayati Benjamin Mkapa

Marais Mwai Kibaki wa Kenya, Yoweri Museveni wa Uganda na Benjamin Mkapa mjini Nairobi baada ya kukamilisha mazungumzo ya kusukuma mbele kuundwa kwa solo la pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki Nairobi August 28, 2004. REUTERS/HO/Kenya Presidential Press Office RSS/THI

Afrika Mashariki inaomboleza kifo cha kiongozi shupavu aliyejitokeza wakati anahitajika kuleta amani katika nchi zenye migogoro na mtu ambaye alileta mageuzi ya kiuchumi Tanzania katika kipindi kifupi.

Wakati Benjamin Mkapa alipochukua madaraka mwaka 1995, wakosoaji wake waliomuona kama mtetezi mkereketwa wa itikadi ya kijamaa ambayo muasisi wa nchi hiyo rais Julius Nyerere alikuwa ameianzisha, limeeleza gazeti la East Africa nchini Kenya.

Wafuatiliaji wa siasa za Tanzania wanasema pamoja na kuwa Mkapa aliendeleza ujamaa, aliazima baadhi ya sera za kibepari ambazo ziligeuza uchumi kuwa bora, ambao ulikuwa umeanguka, na kuaminiwa na taasisi za fedha za kimataifa ambazo ziliondoa mzigo wa madeni kwa nchi hiyo.

Kati ya mambo mengine ambayo Mkapa aliyatekeleza ni kuboresha kukua kwa uchumi wa Tanzania, ni kubinafsisha mashirika ya umma na taasisi za serikali na kuleta mageuzi ya jumla katika ofisi za serikali.

Mkapa alifariki katika hospitali moja mjini Dar es Salaam kutokana na mshtuko wa moyo Alhamisi usiku.

Katika ngazi ya kikanda baada ya kumaliza muda wake wa urais, Mkapa alishiriki kusuluhisha mahasimu wa kisiasa Kenya na Burundi.

Alikuwa ni mjumbe wa jopo la watu mashuhuri lililosimamiwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan ambalo liliunda serikali ya umoja wa kitaifa nchini Kenya baada ya matokeo ya urais yalipozua machafuko na kuuwa watu wasiopungua 1,300.