Harris aahidi kudhibiti uhamiaji na kutozuia upelekaji silaha Israel

Mgombea urais kwa tiketi ya chama cha Demokratik Kamala Harris

Kamala Harris ameahidi kuchukua msimamo mkali juu ya uhamiaji katika eneo la mpaka wa kusini wa Marekani na kusema hatozuia upelekaji silaha kwa Israel.

Amesema hayo katika mahojiano yake ya kwanza na kituo cha habari kikubwa tangu kuwa mgombea urais wa chama cha Demokratik katika mahojiano na kituo cha televisheni cha CNN, jana Alhamisi usiku.

Mahojiano na Harris yaliyofanywa na mtangazaji Dana Bash yaliashiria juhudi yake kuonyesha anasimamia masuala mbalimbali na kuwapa Wamarekani hisia ya namna misimamo yake (Harris) ilivyo katika sera ikiwa imebaki miezi miwili na kitu kufikia Siku ya Uchaguzi Novemba 5.

Harris alisema ataanzisha upya msukumo mpana wa sheria ya mpakani ambayo itaongeza udhibiti wa wahamiaji kuingia Marekani na kuahidi “kutekeleza sheria mbalimbali” dhidi ya uvukaji mpaka.

“Tunazo sheria mbalimbali ambazo lazima zifuatwe na kutekelezwa, zinazo shughulikia na kukabiliana na watu wanaovuka mpaka wetu kinyume cha sheria, na lazima kuwe na kuwajibika,” alisema.

Pia alisema anasimama pamoja na Rais Joe Biden katika uungaji wake mkono kamili kwa Israel na kutupilia mbali wito mbalimbali kutoka kwa Chama cha Demokratik kuwa Washington ifikirie tena juu ya upelekaji silaha Israel kwa sababu ya idadi kubwa ya Wapalestina wanaouwawa huko Gaza.

Alisema anaiunga mkono kikamilifu Israel lakini “lazima sote tufikie makubaliano” kuwezesha kusitishwa mapigano katika vita vya Gaza.

“Hapana, ni lazima tuwezeshe (kufikia sitisho la mapigano na kurejeshwa mateka) kumekamilika.”

Harris alisema haya wakati alipoulizwa iwapo atazuia silaha kupelekwa Israel.