Watu watatu wauawa usiku katika mashambulizi ya mabomu yaliyofanywa na Russia huko Kherson, Kharkiv

Muonekano wa nje wa jengo la makazi ya watu lililoharibiwa na shambulizi la nguvu la mabomu lililofanywa na majeshi ya Russia usiku kucha huko Kherson Agosti. 7, 2023. Picha hii imetokana na video kwa hisani ya Telegram/Oleksandr Prokudin kupitia Reuters

Mwanamke wa Ukraine aliuawa katika mashambulizi yaliyofanywa na Russia mji wa kusini mwa  Ukraine wa  Kherson, maafisa wa eneo walisema

Gavana wa Kherson Oleksandr Prokudin alisema katika ujumbe wake wa Telegram kuwa shambulizi hilo lilianza katikati ya usiku na kuendelea kwa saa kadhaa.

Wakati huo huo, watu wasiopungua wawili waliuawa na wengine watatu kujeruhiwa katika maeneo ya mpakani yaliyoshambuliwa kwa mabomu na Russia katika mkoa wa Kharkiv ulioko kaskazini mashariki mwa Ukraine, Reuters iliripoti, ikimnukuu Andriy Yermak, mkuu wa ofisi ya Rais wa Ukraine.

Andriy Yermak

Shirika la habari linasema wanajeshi 22 wa Ukraine wamerejea nyumbani ikiwa ni sehemu ya matukio ya hivi karibuni ya mabadilishano ya wafungwa siku ya Jumatatu, pia yakimnukuu Yermak.

Yermak alisema wanajeshi walioachiwa ni pamoja na maafisa wawili, masajenti na askari wa kawaida waliokuwa wanapigana katika maeneo tofauti ya mstari wa mbele. Baadhi yao walikuwa wamejeruhiwa.

Katika tathmini yake ya hivi karibuni kuhusu vita vya Ukraine, wizara ya ulinzi ya Uingereza Jumatatu ilisema jeshi la anga la Russia limeendelea kupeleka “vifaa vya kutosha” kuunga mkono operesheni za ardhini huko Ukraine, “lakini bila ya kuwepo athari zozote za operesheni hiyo.”

Ripoti hii imechangiwa na shirika la habari la Reuters.