Rais Ruto kubinafsisha makampuni 35 ya umma

Rais William Ruto wa Kenya

Rais wa Kenya William Ruto amesema Alhamisi serikali ya Kenya inaelekea kubinafsisha makampuni 35 ya umma na ilikuwa inayaangazia makampuni mengine zaidi 100 baada ya kupitisha sheria mwezi uliopita kuondoa urasimu.

Kenya ilibinafsisha kampuni inayomilikiwa na serikali mwaka 2008 wakati ilipotoa IPO kwa asilimia 25 ya hisa katika kampuni ya mawasiliano ya Safaricom.

Mwaka 2009 baraza la mawaziri liliidhinisha orodha ya makampuni 26 kubinafsishwa ikiwa ni pamoja na kampuni ya Kenya Pipeline, kampuni ya uzalishaji umeme, na mabenki lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

“Tumechagua makampuni 35 ambayo yatapelekwa kwa wawekezaji” Ruto aliuambia Mkutano wa maafisa wa soko la hisa la Afrika katika mji mkuu Nairobi.

Hata hivyo Ruto hakuyataja makampuni hayo na waziri wa fedha Njuguna Ndung’u alikataa kufanya hivyo.

Kenya inakabiliana na changamoto kubwa za ukwasi zinazosababishwa na kutokuwa na uhakika juu ya uwezo wake wa kupata ufadhili kutoka kwenye masoko ya fedha kabla ya Eurobond dola bilioni 2 kuwa tayari juni mwakani.