Dunia yaadhimisha miaka kumi ya kifo cha Nelson Mandela

Nelson Mandela alipokuwa akihutubia umati wa watu wakati wa ziara yake ya kuvitembelea vitongoji huko Afrika Kusini Septemba 5, 1990 Picha na AFP/ TREVO

Nelson Mandela alikuwa mwanasiasa wa kimataifa aliyeihamasisha dunia, alikaa jela kwa miaka 27 kwa mapambano yake dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini na baadaye kuwa rais wa kwanza mweusi wa nchi hiyo.

Makomredi wa zamani, wana familia na wachambuzi wanasema Mandela, ambaye alifariki miaka 10 iliyopita, angesikitishwa na hali ilivyo Afrika Kusini hivi leo.

Mandela, ambaye alikuwa anajulikana sana na kupendwa sana Muafrika Kusini, alifariki Desemba 5, 2013, akiwa na umri wa miaka 95.

Mafanikio yake makubwa yalikuwa kuleta uhuru na demokrasia Afrika Kusini na katika chama chake cha African National Congress, au ANC, baada ya miongo kadhaa ya utawala katili wa wazungu wachache.

Aliwasamehe waliokuwa maadui zake na kuanzisha moja ya katiba yenye maendeleo makubwa duniani. Afrika Kusini ilionekana kama mfano wa kimaadili na mwangaza wa matumaini duniani kote.

Mandela alihudumu muhula mmoja madarakani.

Nelson Mandela (katikati), akiwa na naibu wake Walter Sisulu (Kulia) na Katibu Mkuu wa ANC Alfred Nzo huko Boipatong Julai 9, 1991. Picha na WALTER DHLADHLA / AFP

Hata kabla ya kifo chake, alipokuwa amestaafu, chama chake cha ANC kimejikuta kiligubikwa na kashfa za rushwa – hususani chini ya uongozi wa mmoja wa warithi wake, Rais wa zamani Jacob Zuma.

Leo hii, wakosoaji wamekuwa wakikishutumu chama hicho kwa kujali kujilimbikizia utajiri na kushindwa kutoa maisha bora kwa raia wengi maskini wa Afrika Kusini.

Wanasema Madiba, kama alivyojulikana kila mahali, angesikitishwa.

Peter Hain alikuwa rafiki wa Mandela, alimzungumzia mwanaharakati huyo aliyeupinga utawala wa kibaguzi wa rangi ambaye vikosi vya usalama vya utawala huo vilijaribu kumuua kwa bomu la barua mwaka 1972.

"Angeshangazwa sana na uozo nchini, ufisadi uliokithiri unaoendelea, unaowahusisha baadhi ya mawaziri katika Baraza la Mawaziri…. ambao ni wanachama wa chama chake alichokuwa akijivunia cha African National Congress,” Hain alisema.

Vigogo wengine wengi wa ANC na waliokuwepo wakati wa Mandela hawakutaka kutoa maoni yao.

Hata hivyo, mmoja wa wajukuu wa kiongozi huyo, Ndaba Mandela, aliunga mkono maoni kwamba Mandela angesikitishwa sana.