Zelenskyy na viongozi wa NATO na Uingereza wajadili kupata ushindi dhidi ya Russia

Picha iliyotolewa na Ofisi ya Habari ya Rais wa Ukraine Oktoba 10, 2024, akiwemo Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer (Katikati), Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky (Kushoto) na Katibu Mkuu wa NATO Mark Rutte (Kulia).

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy amekutana na viongozi wa Uingereza na NATO mjini London leo Alhamisi kwa mazungumzo yaliyoangazia mpango wa ushindi dhidi ya Russia.

Zelenskyy amekutana na waziri mkuu Keir Starmer na katibu mkuu wa NATO Mark Rutte, kabla ya kusafiri kwenda Paris kwa mazungumzo na rais Emmanuel Macron.

Atafanya mazungumzo na viongozi wa Ujerumani na Italy wiki hii, kujadili mpango huo.

Alikuwa amepangiwa kuwasilisha mpango huo katika mkutano wa wikiendi na viongozi wa nchi za magharibi pamoja na mawaziri wa ulinzi nchini Ujerumani. Mkutano huo umeahirishwa kwa sababu rais wa Marekani Joe Biden amesema analazimika kusalia Marekani ili kufuatilia kimbunga Milton katika ghuba ya Florida.

Rais wa Marekani Joe Biden

Zelenskyy amesema ana matumaini kwamba mkutano huo utapangwa hivi karibuni.