Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Oktoba 10, 2024 Local time: 20:16

Wizara ya ulinzi ya Russia imesema ilitungua Drone 92 za Ukraine


Mfano wa Drones
Mfano wa Drones

Zaidi ya nusu ya ndege hizo zisizo na rubani zilinaswa katika eneo la Krasnodar ambako vifusi vilivyoanguka viliharibu nyumba

Wizara ya Ulinzi ya Russia imesema leo Alhamisi kuwa ulinzi wake wa anga ulitungua ndege 92 zisizo na rubani za Ukraine ambazo zililenga maeneo yaliyo kwenye mpaka wa Russia na Ukraine.

Wizara hiyo imesema zaidi ya nusu ya ndege hizo zisizo na rubani zilinaswa katika eneo la Krasnodar, ambako Gavana Veniamin Kondratyev alisema kuwa vifusi vilivyoanguka viliharibu nyumba kadhaa lakini havikusababisha vifo vyovyote.

Ulinzi wa anga wa Russia pia ulitungua Drone katika mikoa ya Kursk, Rostov, Bryansk, Belgorod na Voronezh, pamoja na kwenye Bahari ya Azov na Crimea inayokaliwa na Russia. Jeshi la Ukraine limesema Alhamisi kuwa limetungua ndege 41 kati ya 62 zisizokuwa na rubani ambazo Russia ilizitumia katika mashambulizi ya usiku kucha.

Uvamizi huo ulifanyika katika mikoa ya Cherkasy, Dnipropetrovsk, Donetsk, Kherson, Kyiv, Mykolaiv, Odesa, Poltava, Sumy na Zaporizhzhia, jeshi la anga la Ukraine limesema. Serhiy Lysak, gavana wa Dnipropetrovsk, alisema kwenye mtandao wa Telegram kwamba shambulio la Russia liliharibu nyumba na bomba la gesi huko Kryvyi Rih, huku likiwajeruhi watu wawili.

Forum

XS
SM
MD
LG