Watanzania waitaka TANESCO kutoa taarifa rasmi kuhusu mgao wa Umeme

fundi umeme akifanya matengenezo katika nguzo ya umeme

Watanzania waitaka TANESCO kutoa taarifa rasmi kuhusu mgao wa Umeme Baadhi ya wananchi nchini Tanzania wamekuwa wakikumbana na changamoto ya mgao wa umeme kwa muda mrefu ambao unaathiri kwa kiasi kikubwa biashara zao na shuguli nyingine za kiuchumi.

Wakizungumza na Sauti ya Amerika, Idhaa ya Kiswahili, baadhi ya Watanzania wamesema mgao wa umeme umekuwa ukisababisha hasara katika biashara zao mara kwa mara. Na wamelitaka shirika la umeme (TANESCO), kutoa taarifa rasmi ya jinsi mgao huo unavyoendeshwa.

Pili Jafari mfanyabiashara wa juisi ya matunda jijini Dar Es Salaam amesema mpaka sasa, hawajui umeme kama ni wa mgao au ni changamoto, na hivyo amelitaka shirika la umeme Tanesco kutoa taarifa rasmi ili waweze kuwaanda wateja wao na kuwapunguzia hasara wanazopata katika biashara zao.

“umeme unatuathiri sana kwasababu mpaka sasahivi hatujui huu umeme ni wa mgao au ni wa vipi afadhali kama muambiwe kama umeme ni wa mgao wajue jinsi ya kujipanga lakini mtu umeshafanya shughuli zako umeshatengeneza juisi zako umetia katika friji mara umeme umekatika baada ya muda unawaka tena ukikaa tena mara umezimika yaani hatuelewi taratibu za umeme zinakwenda vipi” amesema Jafari.

Licha ya ahadi zilizotolewa na watendaji wa serikali kuhusu ongezeko la upatikanaji wa umeme na kutatua tatizo la ukosefu wa umeme bado changamoto ya umeme imeendelea kujitokeza. Hali ambayo inawavunja moyo wananchi na kuondoa uaminifu kwa serikali.

Joshua Lukonge mchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam amesema ni vyema serikali ianze kufikiria vyanzo mbadala vya ugavi umeme kama vile nishati ya jua na gesi kama inavyoshuhudiwa katika mataifa mengine ya Afrika. Na kuwasihi viongozi kuelezea bayana tatizo lililopo na wawajibike kwa wananchi wao.

Aidha amesema “ tuangalie vyanzo vingine kwasababu watu wamekuwa wakishauri kwa muda mrefu unaona cha pili ni viongozi wetu wa kisiasa na watendaji wawe wazi lakini wawe na ufanisi yani wawe na ufanisi sana kwasababu watu hawawezi kusubiri kwa muda mrefu.

Hata hivyo sababu zilizotajwa na TANESCO ni pamoja na mabadiliko ya hali ya hewa ambayo shirika hilo limedai kuwa ndiyo sababibu yaliyopelekea uhaba wa mvua na kupungua kwa kina cha maji katika mabwawa yanayozalisha umeme, na kupelekea kupungua kwa uzalishaji.

Msemaji wa TANESCO, Martine Mwambene, amesema “changamoto ambayo tunayo ni upungufu katika uzalishaji, uzalishaji unatokana pia na kuzalisha umeme kwa njia ya maji ambao vituo vyetu havijapata maji ya kutosha”

Na kuongeza “hizo mvua unazozisema ndio hizo ambazo siyo tunazikosa kwa hiyo ukienda leo Mtera ukifuatilia wewe mwandishi unaweza ukaona kina cha maji kilichopo mwaka wa mwisho Mtera kufurika ilikuwa mwaka 2021 lakini leo maji yanazidi kushuka”.

Aidha amesema kuwa changamoto hiyo kufikia mwakani itakuwa imemalizika baada ya kukamilika kwa mradi wa bwawa la Julius Nyerere lenye uwezo wa kuzalisha megawati 700. Hata hivyo ni muhimu kwa serikali kusimamia utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi na kuhakikisha kuwa unakamilika kwa wakati.

Imetararishwa na Amri Ramadhani VOA Dar es Salaam