Wachambuzi wamurika kukosekana kwa 'mwamba mkubwa...' katika mdahalo wa Warepublikan

Warepublikan wanaowania uteuzi wa kugombea urais Marekani walipofanya mdahalo wao wa kwanza huko Milwaukee, Aug 23 2023 Picha na AP

Mdahalo wa saa mbili, wa kwanza kufanywa na Warepublican katika mzunguko wa uchaguzi huu, ulionyesha mabadilishano yaliyojaa hisia kwa kile ambacho wasimamizi wa mdahalo huo wamekiita, “mwamba mkubwa ambaye hakuwepo hapo,” - ambaye ni mgombea wa mbele, rais wa zamani Donald Trump.

Baadhi ya washindani, kama Makamu Rais wa zamani wa Trump, Mike Pence, na gavana wa zamani wa New Jersey Chris Christie, alimuona Trump hastahili kuongoza tena kwa sababu ya kile alichosema ilikuwa ni kutoiheshimu Katiba, pamoja na zaidi ya makosa 90 ambayo anakabiliana nayo hivi sasa.

Gavana wa zamani wa South Carolina Nikki Haley alitangaza, “Trump ni mwanasiasa ambaye hapendwi sana nchini Marekani. Hatuwezi kushinda katika uchaguzi mkuu kwa njia hiyo”.

Rais wa zamani Donald Trump

Hata hivyo, mwanasiasa chipukizi Vivek Ramaswamy, akiwa anapanda katika maoni, alisimama na Trump, akisema anaamini alikuwa ni “ni rais bora wa karne ya 21.”

Ramaswamy pia alisimama mbali katika kuhoji uungaji mkono wa Marekani kwa Ukraine, akisema China ni tishio kubwa kwa Marekani kuliko Russia. Wagombea wengine kadhaa, akiwemo Nikki Haley, pia balozi wa zamani wa Marekani kwenye Umoja wa Mataifa, alielezea uungaji mkono wake wa dhati kwa Ukraine kujitetea dhidi ya majeshi ya Russia.

Baada ya mdahalo, Pence aliwaambia waandishi wa habari kuwa mtu yeyote asishangazwe na nguvu yake kwenye jukwaa la mdahalo.

“Nilikuwa bingwa wa thamini za kiconservative katika utawala wa Trump na Pence. Najua jinsi ya kupigana na nina furaha ya kuleta mapambano haya hivi leo,” amesema Mike Pence.

Mpinzani mkuu wa Pence jana usiku alikuwa Ramaswamy, alisema alifurahishwa na malumbao ya maneno yaliyoelekezwa kwake na makamu rais wa zamani.

Ramaswamy amesema “Mike Pence ananijia mimi kwa ujuzi wake tofauti, nadhani hiyo ni jambo zuri kwasababu sidhani watu katika nchi hii wana hamu ya kurudi kwa watu ambao wanazungumzia kauli mbiu walizokariri mwaka 1980.”

Warepublcian watafanya mdahalo wao wa pili mwezi ujao huko California. Lakini mmoja wa wagombea atarejea katika jukwaa hili hili hapa Wisconsin mwaka ujao mwezi Julai kwa ajili ya uteuzi wa chama.

Habari hii imechangiwa na vyanzo mbalimbali vya habari.