Kiongozi mpya wa Intelijensia wa Misri ateuliwa

Rais wa Misri ,Abdel Fattah al-Sisi.

Rais wa Misri Abdel Fattah al Sisi Jumatano ameteua Meja Jenerali Hassan Mahmoud Rashad, kuwa mkuu wa Idara yenye nguvu ya Intelijensia, akichukua nafasi ya Abbas Kamel ambaye sasa atakuwa mshauri wa Rais.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, Idara hiyo chini ya utwala wa Sisi imekuwa ikitekeleza majukumu ya sera za kigeni ikiwemo mizozo ya Gaza, Sudan na Libya, pamoja na masuala ya usalama wa ndani ambao umehusishwa na misako dhidi ya wapinzani wa kisiasa.

Rashad awali alikuwa naibu wa Kamel, na kulingana na vyanzo viwili vya usalama, amechukua usukani wa masuala muhimu ikiwemo kuimarisha uhusiano kati ya Misri na Iran. Kamel mwenye umri wa miaka 68 aliteuliwa mkuu wa Idara ya Intelijensia 2018, na kabla ya hapo alikuwa kwenye intelijensia ya kijeshi na pia mratibu kwenye ofisi ya Rais.

Katika siku za karibuni ameombwa kugawa kazi kutokana na changamoto za kiafya.Mazungumzo yaliokwama ya sitisho la mapigano ya Gaza, na ambayo Misri imekuwa mmoja wa wapatanishi pamoja na Marekani na Qatar yamekuwa yakiongozwa na afisa mwingine wa nagazi ya juu wa intelijensia , akisimamiwa na Kamel. Picha zilizotolewa pamoja na taarifa Jumatano zimeonyesha Rashad na Kamel wakikutana na Rais Sisi, huku Rashad akikula kiapo mbele yake.