Marekani kutoa msaada wa zaidi ya dola milioni 400 kwa DRC

Wanajeshi wa Congo wakifanya doria katika kijiji cha Mwenda kilichoko Kaskazini Mashariki mwa DRC. Picha ya maktaba na ALEXIS HUGUET / AFP.

Marekani imesema Jumatano kwamba itatoa karibu dola milioni 414 kwa ajili ya misaada  ya kibinadamu kwa Jamhuri ya Kidemokarasi ya Congo, ambako zaidi ya watu milioni 25 wanahitaji misaada hiyo, ikiwa ni takriban robo ya wakazi nchini humo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, balozi wa Marekani kwenye Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, Jeffrey Prescott, amesema kuwa fedha hizo zitakwenda kwa mashirika ya UN, yanayotoa misaada ya haraka ya chakula, huduma za afya na lishe bora, makazi, maji na usafi.

Ufadhili huo pia unajumuisha vifaa vya moja kwa moja vya killimo kutoka kwa wakulima wa Marekani, amesema Prescott, ambaye atatangaza rasmi msaada huo mjini Kinshasa akiwa na balozi wa Marekani nchini DRC, Lucy Tamlyn.

Prescott amesema kuwa hatua hiyo inafikisha misaada ya Marekani kuwa jumla ya dola milioni 838 tangu Oktoba mwaka jana. Jeshi la Congo limekuwa likipambana na waasi wa M23 tangu 2022, na mapigano mapya mashariki mwa nchi yamewasukuma zaidi ya watu milioni 1.7 kutoroka makwao, na kufikisha jumla ya idadi ya watu waliotoroka makwao kuwa milioni 7.2 tangu ghasia zilipozuka.