Jaji aidhinisha dhamana ya $200,000 ya Trump

Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump (Katikati)

Jaji mmoja wa Georgia, Jumatatu aliidhinisha dhamana  ya dola 200,000 kwa rais wa zamani Donald Trump katika kesi ya ulaghai iliyowasilishwa dhidi yake katika jimbo hilo la kusini mwa Marekani.

Trump na wengine 18 katika kesi hiyo ya kihistoria wamepewa hadi saa sita mchana siku ya Ijumaa kujisalimisha kwa mamlaka huko Georgia ili kusomewa mashtaka.

Mbali na dhamana hiyo, Jaji wa Mahakama ya Kaunti ya Fulton Scott McAfee aliweka masharti kadhaa katika makubaliano yaliyoidhinishwa na waendesha mashtaka na mawakili wa Trump.

"Mshtakiwa hatafanya kitendo chochote cha kumtisha mtu yeyote anayejulikana kwake kuwa mlalamishi au shahidi katika kesi hii au kuzuia utoaji wa haki kwa njia yoyote," McAfee alisema katika uamuzi wa mahakama wa kurasa tatu.

Alisema vitisho kama hivyo vitajumuisha kuchapisha jumbe za mitandao ya kijamii, au kutuma vitisho kama hivyo vikiwa vimechapishwa na mtu mwingine..

McAfee aliweka dhamana ya dola 100,000 kwa kila mmoja kwa washitakiwa wengine wawili katika kesi hiyo -- mawakili wa zamani wa kampeni ya Trump John Eastman na Kenneth Chesebro.