Idadi ya vifo katika tetemeko la ardhi China yaongezeka, wengine hawajulikani walipo

Eneo la Jimbo la Qinghai lililokumbwa na tetemeko la ardhi nchini China.

Idadi ya vifo kutokana na tetemeko kubwa la ardhi China ambalo halijatokea kwa miaka mingi imeongezeka kufikia 149, huku watu wawili wakiwa hawajulikani waliko baada ya tetemeko hilo kupiga sehemu za kaskazini magharibi mwa nchi hiyo wiki iliyopita.

Tetemeko la kiwango cha 6.2 kwa kipimo cha rikta lilipiga eneo la ndani zaidi la milimani kati ya majimbo ya Gansu na Qinghai Desemba 18, na kuzigeuza nyumba kuwa vifusi na kusababisha maporomoko makubwa ya matope ambayo yalivikumba vijiji viwili katika jimbo la Qinghai.

Shirika la utangazaji la serikali la CCTV lilisema Jumatatu idadi ya vifo katika mji wa Donghai huko Qinghai imeongezeka kwa mtu mmoja, kufikia 32, na waokoaji walikuwa bado wanawatafuta watu wawili waliotoweka. Katika eneo jirani la Gansu, mamlaka ziliripoti vifo vya watu 117.

Takriban watu 1,000 walijeruhiwa na nyumba zaidi ya 14,000 ziliharibiwa katika tetemeko lililouwa zaidi China katika kipindi cha miaka tisa.

Shule za msingi katika kaunti ya Jishishan huko Gansu zilianza tena masomo katika mahema Jumatatu, shirika la habari la serikali liliripoti.

Mamlaka za eneo zimesema zitatumia kipindi cha mapumziko ya majira ya baridi kinachokuja kukarabati shule zilizoharibiwa na kujenga majengo ya muda ili madarasa yaweze kuanza kama kawaida kipindi cha machipuko.

Majengo yaliyo haribiwa na tetemeko huko Dahejia, Kaunti ya Jishishan kaskazini magharibi jimbo la Gansu, China Disemba 19, 2023. (Photo by Pedro Pardo / AFP)

Mamlaka husika ziliharakisha kujenga nyumba kadhaa za muda kwa ajili ya manusura wanaokabiliwa na baridi ambayo viwango viko chini sana.

CGTN, kitengo cha kimtaifa katika shirika la utangazaji la serikali, kilisema idadi ya kwanza ya nyumba za muda 500 zimeshajengwa kwa ajili ya wakazi huko Meipo, kijiji kimoja kilichopo Gansu, usiku wa Ijumaa.

Zaidi ya watu 87,000 wamepatiwa makazi baada ya tetemeko hilo.

Tetemeko hilo lilisababisha hasara ya kiuchumi iliyokadiriwa kuwa na thamani ya milioni ya dola za Kimarekani katika sekta za kilimo na uvuvi, kulingana na vyombo vya habari vya serikali.

Chanzo cha habari hii ni shirika la habari la AP.