China yakataa wito wa Marekani wa kuimarishwa kwa mawasiliano ya kijeshi

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken na rais wa China Xi Jinping.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken alikutana Jumatatu na Rais wa China Xi Jinping na kusema walikubaliana "kuimarisha" uhusiano uliozorota vibaya kati ya Marekani na China, lakini mwanadiplomasia huyo mkuu wa Marekani aliondoka Beijing huku pendekezo lake kuu lilikataliwa.

Marekani ilikuwa imetoa wito wa kuimarishwa kwa mawasiliano ya moja kwa moja ya kijeshi.

Baada ya kukutana na Xi, Blinken alisema China haiko tayari kuanzisha tena mawasiliano ya jeshi kwa jeshi, jambo ambalo Marekani inaona kuwa muhimu ili kuepuka hali ya kutoelewana na ongezeko al migogoro, hasa kuhusu Taiwan.

Hata hivyo, mwanadiplomasia mkuu wa China anayehusika na masuala ya mataifa ya Magharibi, Yang Tao, alisema alifikiria ziara ya Blinken nchini China "inaashiria mwanzo mpya."

"Upande wa Marekani kwa hakika unafahamu kwa nini kuna ugumu katika mawasiliano ya kijeshi," alisema, akilaumu vikwazo vya Marekani moja kwa moja, ambavyo Blinken alisema vinahusu vitisho kwa usalama wa Marekani.

Hata hivyo Blinken na Xi walijitangaza kuwa wameridhika na maendeleo yaliyopatikana katika siku mbili za mazungumzo, bila kuashiria maeneo maalum ya makubaliano, zaidi ya uamuzi wa pande zote wa kurejelea ajenda pana ya ushirikiano na ushindani iliyoidhinishwa mwaka jana na Xi na Rais Joe Biden katika mkutano wao mkuu, uliofanyika mjini Bali, Indonesia.