Biden kujadili mzozo wa Mashariki ya Kati pembezoni mwa Mkutano wa Baraza Kuu la UN

Biden delivers remarks at the Economic Club of Washington DC

Rais Joe Biden anatarajiwa kutoa hotuba yake ya mwisho kama kiongozi wa Marekani mbele ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wiki hii.

Lakini suala moja muhimu wakati anapokutana pembezoni, na viongozi wengine huko New York, ni mzozo wa Mashariki ya Kati - na jinsi sera za utawala wake zimeushughulikia.

Hii ni mara ya mwisho kwa Rais Joe Biden kuhutubia kongamano hilo kuu la kimataifa: ambapo mamia ya viongozi wanakusanyika kila mwaka kwa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Haya yanajiri katika wakati mgumu, anasema balozi wa Marekani katika shirika hilo la kimataifa.

Linda Thomas-Greenfield ni balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa anaeleza: "Tunasema hivi kila mwaka, lakini mkutano huu wa UNGA unafanyika katika wakati mgumu zaidi na wenye changamoto zaidi. Orodha ya migogoro ambayo inahitaji umakini na hatua, inaonekana kuongezeka kila uchao."

Linda Thomas-Greenfield

Suala la kwanza kwenye orodha hiyo, ni Gaza. Hapa, msimamo wa Marekani hauwiani na wa wajumbe wengine kwenye baraza hilo, ambalo wiki iliyopita lilipitisha kwa wingi wa kura, azimio la kuitaka Israel ikomeshe hatua ya kukalia kwa mabavu eneo la Palestina ndani ya miezi 12 ijayo.

Marekani ilikuwa miongoni mwa nchi 14 zilizopiga kura ya "hapana", ambazo Thomas-Greenfield alisema ziliendana na msimamo wa Washington kuhusu "hatua za upande mmoja ambazo zinadhoofisha matarajio ya suluhisho la serikali mbili."

Wachambuzi wanatarajia Biden kujadili msaada wake kwa Israel na uungaji mkono wake kwa Ukraine katika hotuba ya mwaka huu. Wanaangazia migogoro hiyo miwili kama changamoto kuu anapomaliza urais wake.

Jim Kessler wa Taasisi ya Third Way anaeleza: "Pamoja na Mashariki ya Kati, unawezaje kulifunikia hili na utumai kuwa mzozo hautakuwa mkubwa na kuwa vita vya kikanda? Na nadhani huo ndio ubashiri wa wengi kuhusu kile kitakachotokea.”

Baraza la Usalama la UN likijadili hali ya Mashariki ya Kati huko New York, Aprili 14, 2024.

Jambo moja liko wazi, kwa masikitiko: mzozo unapokaribia kufikia mwaka mmoja, karibu mateka 100 wanadhaniwa kusalia chini ya ulinzi wa Hamas. White House inasema kuwarejesha nyumbani ndicho kipaumbele kikuu, na ni nguzo muhimu ya makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Israel na kundi hilo la wanamgambo.

Kessler anasema viongozi wengi watamkaribisha Biden kwa shangwe wakati wa hotuba yake, kwa sababu ametumia muda wake kujenga upya miungano na kurejesha kanuni za kimataifa.

Anaongeza kuwa:"Anapendwa huko nje katika mataifa mengi. Bila shaka, kuna wachache ambao hawapo kwenye kundi hilo.”

Biden atahutubia kongamano hilo mjini New York kesho Jumanne.