Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatatu, Julai 01, 2024 Local time: 18:29

Wairan kufanya duru ya pili ya uchaguzi Julai 5


Upigaji kura nchini Iran.
Upigaji kura nchini Iran.

Iran itafanya duru ya pili ya uchaguzi wa rais ili kuamua ni nani atachukua nafasi ya rais wa zamani marehemu Ebrahim Raisi, afisa mmoja alisema Jumamosi, baada ya duru ya kwanza ya zoezi hilo, lililofanyika Ijumaa, kutobaini mshindi wa moja kwa moja.

Uchaguzi wa Ijumaa wiki ijayo utawajumuisha mgombea mpenda mageuzi Masoud Pezeshkian dhidi ya mgombea mwenye msimamo mkali na aliyekuwa mtetezi wa mpango wa nyuklia wa Iran, Saeed Jalili.

Mohsen Eslami, msemaji wa tume ya uchaguzi alitangaza matokeo hayo katika mkutano na waandishi wa habari uliopeperushwa na televisheni ya taifa ya Iran.

Alisema kati ya kura milioni 24.5 zilizopigwa, Pezeshkian alipata milioni 10.4 huku Jalili akipata milioni 9.4. Spika wa Bunge Mohammad Bagher Qalibaf alipata milioni 3.3, huku kiongozi wa dhehebu la Kishia Mostafa Pourmohammadi akipata zaidi ya kura 206,000.

Sheria za Iran zinahitaji kwamba mshindi apate zaidi ya asili mia 50 ya kura zote zilizopigwa. Ikiwa sivyo, wagombeaji wawili bora wa kinyang'anyiro hicho, watafuzu kwa duru ya pili wiki moja baadaye.

Kumekuwa na uchaguzi mmoja tu wa marudio wa urais katika historia ya Iran: mwaka 2005, wakati Mahmoud Ahmadinejad mwenye msimamo mkali alimshinda Rais wa zamani Akbar Hashemi Rafsanjani.

Eslami alikiri Baraza la Walinzi la nchi hiyo litahitaji kutoa idhini rasmi, lakini matokeo ya awali hayakuleta changamoto yoyote ya haraka kutoka kwa wagombea katika kinyang'anyiro hicho.

Kama ambavyo imekuwa tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya 1979, wanawake na wale wanaotaka mabadiliko makubwa wamezuiwa kugombea, na waangalizi wanaotambuliwa kimataifa hawaruhusiwi kuwepo.

Forum

XS
SM
MD
LG