Wanajeshi nane wa Israel wauwawa Lebanon

  • VOA News

Mwangaza ukipaa angani kufuatia mashambulizi ya Israel ndani ya Lebanon.

Jeshi la Israel limesema Jumatano kwamba wanajeshi wake 8 wameuwawa kwenye mapigano yanayoendelea dhidi ya wanamgambo wa Hezbollah, kusini mwa Lebanon, siku moja baada ya kuanza kile kilochotajwa kuwa operesheni maalum ya ardhini inayolenga kuharibu miundombinu ya kundi hilo.

“Tupo kwenye vita vikali dhidi ya kundi la Iran linalopanga kutuangamiza,” alisema Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu. “Hilo halitawezekana kuwa tutasimama pamoja na kushinda, Mungu akiwa nasi,” aliongeza kusema.

Jeshi la wanahewa la Israel lilifanya mashambulizi ya anga usiku kucha kwenye ngome za Hezbollah, kusini mwa mwa mji mkuu wa Lebanon, Beirut. Jumanne, wizara ya afya ya Lebanon ilisema kuwa takriban watu 55 waliuwawa na wengine 156 kujeruhiwa kwenye mashambulizi ya Israel ndani ya saa 24 zilizopita.

Idadi hiyo inajumuisha raia na wanajeshi. Hali ya taharuki imeendelea kuongezeka tangu Jumanne jioni, kufuatia mashambulizi ya makombora takriban 200 yaliorushwa na Iran ndani ya Israel. Iran ilifanya mashambulizi hayo wakati wa mkesha wa Siku Kuu ya Mwaka Mpya ya Wayahudi, yakiwa ya kulipiza kisasi cha mashambulizi kutoka Israel , yaliouwa viongozi kadhaa wa kipalestina ndani ya Labanon.