Vita nchini Ukraine na Gaza vimeathiri sherehe za mkesha wa mwaka mpya 2024

Watu wajitokeza kusherehekea mwaka mpya huko Jijini New York, Marekani katika mkesha wa kuamkia tarehe 01.01.2024.

Vita nchini Ukraine na Gaza vimeathiri sherehe za mkesha wa Mwaka Mpya kwa namna mbalimbali. Miji mingi duniani iliongeza ulinzi na baadhi ya sehemu walifuta  sherehe hizo  kwa jumla.

Wakati matamasha ya mkesha wa Mwaka Mpya yalikuwa mengi kote nchini Marekani Jumapili usiku, mwandishi maarufu wa habari wa Kituo cha Televisheni cha CNN Anderson Cooper alifuatilia salamu za rambirambi zilizotolewa kwa watumbuizaji mbalimbali waliofariki mwaka 2023 kwa kukiri kuwa programu yenye kufurahisha ya kilele cha mwaka mpya akiwa na mwendesha mwenza wa kipindi Andy Cohen kuwa inaweza kuwa ni tukio la kusikitisha kwa baadhi ya watazamaji.

“Kuna watu wengi ambao wanahisi hawawezi kusherehekea,” alisema katika dakika za mwisho za kumalizika mwaka 2023 ambazo zilimpoteza Tina Turner, Tony Bennett, Harry Belafonte, Sinead O’Connor, Jimmy Buffet, Burt Bacharach na David Crosby, kati ya wengine.

Fataki Zafanya Usiku Ung’are

Shamrashamra za fataki za ajabu zilishamiri katika maeneo mbalimbali maarufu ya dunia kama vile Acropolis huko Athens, Ugiriki; Zilionekana katika jumba la vioo refu sana duniani, Burj Khalifa, huko Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu; na kuambatana na nderemo ambazo zilitawala katika anga huko Nairobi, Kenya.

Papa Aainisha Gharama ya Maisha ya Binadamu katika Vita

Huko Vatican, Papa Francis alikumbusia mwaka 2023 kuwa ni mwaka ulioweka kumbukumbu ya mateso ya vita. Katika maombi ya baraka ya kila Jumapili kutoka kwenye dirisha mojawapo linaloelekea Viwanja vya St. Peters, alifanya maombi kwa “watu wa Ukraine wanaoteseka na Wapalestina na Waisraeli, watu wa Sudan na wengine wengi.”

“Mwisho wa mwaka, tutakuwa na ushujaa wa kujiuliza ni maisha ya watu wangapi yameathiriwa na vita vya silaha, wangapi wamekufa na kiwango gani cha uharibifu, kiwango cha mateso, na kiwango cha umaskini unaotokana na vita hivi,” papa alisema.

Vita vya Gaza na Ukraine Vinaendelea

Huko Russia, hatua za kijeshi zinazochukuliwa na nchi hiyo dhidi ya Ukraine ziligubika tafrija mbalimbali za mwisho wa mwaka, huku sherehe za kurusha fataki na maonyesho katika viwanja vya Red Square huko Moscow zilifutwa kama ilivyokuwa mwaka uliopita.

Mashambulizi ya Israel

Mashambulizi ya Israeli huko Ukanda wa Gaza yaliua watu wasiopungua 35 Jumapili, maafisa wa hospitali walisema, huku vita vikiendelea katika eneo lote katika eneo finyu siku moja baada ya Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu, kukataa wito wa kimataifa wa kusitisha vita, akisema kuwa vita vitaendelea kwa “miezi mingi ijayo.”

Majengo marefu mjini Tel Aviv yalikuwa yamewashwa taa za njano kupaza sauti ya kutaka kuachiliwa kwa mateka wanaoshikiliwa na wapiganaji wa Hamas huko Gaza kwa zaidi ya siku 80.

“Wakati unahesabu kumalizika kwa mwaka uliopita na kuingia mwaka mpya, nyakati zetu na maisha yetu yamesimama,” alisema Moran Betzer Tayar, ndugu wa mama yake Yagev Buchshtab, mwenye umri wa miaka 34 anayeshikiliwa mateka.

Wapalestina Gaza

Huko Ukanda wa Gaza, Wapalestina waliolazimika kukimbia makazi yao walijikusanya pembeni ya moto katika makazi ya muda ya kambi ya wakimbizi.

“Kutokana na ukubwa wa madhila tunayoishi nayo, hatuhisi kama kuna mwaka mpya,” alisema Kamal al-Zeinaty, ambaye amepoteza wanafamilia wengi katika vita hivyo. “Siku zote ziko sawa.”

Wakristo nchini Iraq

Huko Iraq, mti wa Krismas ulipambwa na bendera za Palestina na miili bandia ya watu ikiwa na sanda, pembeni ya mlingoti wa uhuru katikati ya Baghdad.

Wakristo wengi nchini Iraq wamesitisha sherehe za mwaka huu kwa kuwaunga mkono wananchi wa Gaza, na wamechagua kufanya sherehe zao kwa maombi na ibada nyingine.

“Tunatumai kuwa mwaka mpya, 2024, utakuwa ni mwaka wa mema, mafanikio na furaha,” alisema Ahmed Ali, mkazi wa Baghdad.

Chanzo cha habari hii ni Shirika la Habari la AP na vyanzo vingine.