Russia yashambulia kwa makombora hospitali ya wazazi, yaua 13 na kujeruhi 18

Wafanyakazi wa idara ya zimamoto wakipambana kuzima moto uliosababishwa na shambulizi la Russia huko Kharkiv, Ukraine, Dec. 29, 2023.

Russia imefanya wimbi la mashambulizi ya makombora katika miji kadhaa ya Ukraine Ijumaa, ikiuua watu wasiopungua 13 na kujeruhi wengine wasiopungua 18, maafisa wa Ukraine walisema. Mamlaka zilisema kuwa idadi ya vifo inatarajiwa kuongezeka.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy alibandika katika mtandao wa X, uliokuwa unajulikana kama Twitter: “Leo, Russia imetumia takriban kila aina ya silaha zake: ‘Kindzhals,’ S-300s, makombora ya masafa marefu, na droni kadhaa. … Jumla ya kiasi cha makombora 110 yalipigwa dhidi ya Ukraine, huku mengi kati ya hayo yalitunguliwa.”

Zelenskyy alisema hospitali ya wazazi ni kati ya maeneo yaliyolengwa na shambulizi la Russia. Maeneo mengine yaliyolengwa ni pamoja na “majengo ya elimu, maeneo ya biashara, maghorofa kadhaa ya makazi ya watu na nyumba za watu binafsi, ghala za biashara na eneo la kuegesha magari.”

Miji ambayo ilipigwa na shambulizi la Russia, kulingana na posti ya Zelens kyy ni pamoja na Kyiv, Lviv, Odesa. Dnipro, Kharkiv na Zaporizhzhia.

Milipuko hiyo ilisikika kote katika mji mkuu wa Ukraine mapema Ijumaa na meya Vitali Klitschko aliwashauri wakazi wa Kyiv kutafuta hifadhi. Gazeti la Kyiv Independent linaripoti makombora sita yalilipuka huko Kharkiv na milipuko mengine kutokana na droni zilizopiga Lviv.

Katika posti ya mtandao wa Telegram, meya wa Kharkiv Igor Terekhov alieleza shambulizi hilo kuwa ni “ ni shambulizi kubwa la makombora.”

Lviv Mayor Andriy Sadovyi aliposti katika Telegram kuwa mji wake ulishambuliwa angalau mara mbili.

Zelenskyy alisema alijadili fomula ya amani ya Ukraine alipozungumza kwa simu na Papa Francis siku ya Alhamisi.

“Tulijadili ushirikiano wetu katika kuweka Formula ya Amani ya Ukraine kivitendo,” Zelenskyy alisema katika posti yake aliyobandika kwenye mtandao wa X, uliokuwa ukijulikana kama Twitter.

“Zaidi ya nchi 80 tayari zinajihusisha na mchakato huu kwa kiwango cha wawakilishi wao. Na kutakuwa na wengine zaidi watakao jiunga nao,” alisema.

Katika ujumbe wa papa wa Siku ya Krismas, alitoa wito wa kumalizwa vita vya Ukraine, kati ya migogoro mingine inayoendelea.

Baadhi ya taarifa katika ripoti hii imetokana na mashirika ya habari ya AP, AFP na Reuters.