Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Septemba 28, 2024 Local time: 16:23

India yapinga madai ya China ya umiliki wa maeneo yenye mivutano


Ramani inayoonyesha mipaka ambayo ina mivutano kati ya China na India.
Ramani inayoonyesha mipaka ambayo ina mivutano kati ya China na India.

India ilisema Jumanne ilikuwa imewasilisha  “pingamizi kali” dhidi ya China siku moja baada ya Beijing kutoa ramani mpya ya mwaka 2023 ikionyesha Aksai Chin – eneo la Kashmir ambalo kwa kiasi kikubwa linadhibitiwa na China

Ramani hiyo pia inaonyesha jimbo la kaskazini mashariki la India la Arunachal Pradesh likiwa katika ardhi ya ndani ya eneo la China

Ramani hiyo ilitolewa Jumatatu katika tovuti inayoonyesha ramani rasmi ya Wizara ya Mali ya Asili ya China, siku kadhaa baada ya mataifa hayo mawili kukubaliana kufanya kazi kwa pamoja kupunguza mivutano inayohusu mipaka yao.

Ramani hiyo pia inajumuisha Taiwan na bahari ya South China Sea kuwa ni eneo la China.

Siku ya Jumanne jioni, Wizara ya Mambo ya Nje ya India ilitangaza kuwa imewasiliana na wizara husika ya China kupinga hatua hiyo.

“Leo tumepeleka pingamizi kali kupitia mfumo wa kidiplomasia kwa upande wa China kwa kile wanachokiita ramani rasmi ya 2023 ya China ambayo inadai kumiliki eneo la India,” msemaji wa wizara Arindam Bagchi alisema.

Ni wiki iliyopita tu, Waziri Mkuu Narendra Modi na kiongozi wa China Xi Jinping walikutana katika mkutano wa viongozi BRICS Afrika Kusini na kukubaliana “kuzidisha juhudi” za kupunguza mivutano ya mipakani. Nchi zote mbili zilitangaza makubaliano hayo kama ni hatua ya kuboresha uhusiano wao.

Kutolewa kwa ramani hiyo kunakuja kabla ya mkutano wa kimataifa wa G20 au mkutano wa kikundi cha mataifa 20, India ni mwenyeji wa mkutano huo ambao utafanyika New Delhi Septemba 9 na 10 na umepangwa kuhudhuriwa na Xi na viongozi wengine wa dunia.

Manish Tewari, mbunge kutoka chama cha upinzani cha Congress, alisema Jumanne kuwa Serikali ya Modi ifikirie kwa makini iwapo itamkaribisha Xi katika mkutano huo.

Forum

XS
SM
MD
LG