Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Oktoba 23, 2024 Local time: 06:28

Balozi wa Ufaransa awasili Paris kufuatia kufukuzwa na utawala wa kijeshi nchini Niger


Polisi wa doria nchini Niger wakipita kwenye ubalozi wa Ufaransa huko Niamey tarehe 28 Agosti, 2023. Picha na AFP.
Polisi wa doria nchini Niger wakipita kwenye ubalozi wa Ufaransa huko Niamey tarehe 28 Agosti, 2023. Picha na AFP.

Balozi wa Ufaransa nchini Niger Sylvain Itte amewasili mjini Paris Jumatano, baada ya wiki kadhaa za mivutano na utawala wa kijeshi uliomfukuza nchini humo kufuatia mapinduzi katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa Catherine Colonna alikutana na Itte " kumshukuru yeye na timu yake kwa kulitumikia taifa letu katika mazingira magumu," wizara hiyo ilisema katika taarifa iliyoandikwa kwa shirika la habari la AFP.

"Balozi na wenzake sita waliondoka Niamey majira ya saa kumi asubuhi” chanzo cha habari cha kidiplomasia kutoka ubalozi wa Ufaransa kilisema.

Balozi huyo wa Ufaransa nchini Nigeria, alizaliwa katika mji mkuu wa Mali Bamako mwaka 1959. Alishika wadhifa huo wa ubalozi nchini Niger kwa muda wa mwaka mmoja.

Amekuwa akifanya kazi za kidiplomasia kwa muda wa miaka 35, na kabla ya hapo alikuwa balozi wa Uruguay na Angola.

Uhusiano kati ya Niger na Ufaransa, mtawala wa zamani wa kikoloni ambaye alidumisha uwepo wa kijeshi nchini humo kwa lengo la kupambana na waasi wa kundi la Kiislamu, umevunjika tangu maafisa wa jeshi kuchukua madaraka huko Niamey mwezi Julai.

Utawala wa kijeshi ulimuamuru balozi wa Ufaransa Sylvain Itte kuondoka nchini humo ndani ya saa 48 mwishoni mwa mwezi Agosti , kutokana na kile walichokieleza kuwa ni vitendo vya Ufaransa vilivyokuwa "kinyume na maslahi ya Niger."

Awali Ufaransa ilipuuzia agizo hilo, ikishikilia msimamo wake kwamba serikali ya kijeshi haikuwa halali na kutaka kurejeshwa madarakani kwa Rais mteule Mohamed Bazoum, aliyepinduliwa mwezi Julai.

Tangu jeshi lichukue madaraka, kumekuwa na maandamano takriban kila siku yakupinga uwepo wa Ufaransa huko Niamey. Umati wa wafuasi wa utawala wa kijeshi wametumia siku kadhaa kuweka kambi nje ya makao ya kijeshi ya Ufaransa wakidai kuondoka kwa wanajeshi hayo.

Chanzo cha habari hii ni Shirika la habari la AFP na Reuters

Forum

XS
SM
MD
LG