UN yaondoa baadhi ya maafisa wake Haiti

waandamanaji wakichoma moto mataili huko Port-au-Prince Machi 12, 2024. Picha na AFP

Umoja wa Mataifa umeanza kuwaondowa wafanyakazi wake wasio na majukumu muhimu nchini Haiti kutokana na kuongezeka kwa ghasia na ukosefu wa usalama katika taifa hilo la Caribean.

Msemaji wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric amewambia waandishi habari Jumatano jioni kwamba Umoja wa Mataifa hauondoki nchini humo na kwamba watumishi wake wanaofanya kazi za kuokoa maisha wataendelea na operesheni zao.

Tangu Februari 29 magenge ya uhalifu huko Haiti yalianzisha mashambulio dhidi ya majengo ya umma katika mji mkuu wa Port-au-Prince, ikiwa ni pamoja na vituo vya polisi na uwanja wa ndege wa kimataifa na kumtaka waziri mkuu Ariel Henry kujiuzulu.

Henry alitangaza mapema wiki hii kwamba atajiuzulu mara baada ya serikali ya mpito itakapotangazwa.