Ukraine yapinga ombi la Papa Francis kujadili kusitisha vita na Russia

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Papa Francis

Ukraine Jumapili ilipinga wito wa Papa Francis wa kujadili kusitisha vita na Russia, huku Rais Volodymyr Zelenskiy akisema Papa alikuwa akifanya “upatanishi kwa mbali” na waziri wake wa mambo ya nje akisema Kyiv haitasalimu amri.

Francis alisema kuwa wakati mambo yanaelekea kubaya kwa pande kwenye mzozo, mtu anapaswa kuonyesha “ujasiri wa kusalimu amri kwa kuinua bendera nyeupe” na kujadiliana.

Mahojiano ya Papa yaliaminika kuwa ni mara ya kwanza kutumia maneno kama “kuinua bendera nyeupe” au “kushindwa” kwa kujadili vita vya Ukraine, ingawa aliwahi kutaja umuhimu wa mazungumzo.

Zelenskiy hakutaja moja kwa moja Francis au maoni yake lakini alitaja wanadini wanaosaidia ndani ya Ukraine.

“Wanatuunga mkono kwa maombi, kwa majadiliano yao na kwa vitendo. Hivi ndivyo kanisa lenye watu lilivyo,” Zelenskiy alisema katika ujumbe wa kila usiku kupitia video.

Waziri wa mambo ya nje Dmytro Kuleba, akiandika kwenye mtandao wa X alisema kuwa mtu mwenye nguvu katika mzozo wowote “husimama upande wa wema badala ya kujaribu kuwaweka wote kwenye kigezo sawa na kuyaita “mazungumzo’.

“Bendera yetu ni ya njano na bluu,” Kuleba aliandika kwa Kiingereza, akimaanisha bendera ya taifa ya Ukraine.

Hiyo ndiyo bendera inafanya tunaishi, kufa na kushinda. Hatutainua hata siku moja bendera nyingine yoyote.”