Rais wa Marekani Donald Trump Jumapili alisema anaamini Marekani imepiga hatua katika mazungumzo ya kumaliza vita kati ya Russia na Ukraine, lakini hakutoa maelezo yoyote kuhusu mawasiliano kati yake na Rais Vladimir Putin.
Akizungumza na waandishi wa habari akiwa ndani ya Air Force One, Trump alidokeza kuwa yeye na Putin wamekuwa wakiwasiliana, na yatakuwa mazungumzo ya kwanza kutambuliwa rasmi kati ya Putin na Rais wa Marekani tangu mapema mwaka wa 2022.
Alipoulizwa kama amekwisha zungumza na Putin tangu awe rais Januari 20 au kabla, Trump alisema “Nimefanya mazungumzo naye. Wacha tuseme nimezungumza naye. Na ninatarajia kufanya naye mazungumzo zaidi. Tunapaswa kumaliza vita hivyo.”
Trump alisema Marekani inaendelea kuwasiliana na Russia na Ukraine. “Tunazungumza na pande zote mbili,” alisema.