Russia yaanza zoezi la kuandikisha maelfu ya wanajeshi wapya

  • VOA News

Wanajeshi wa Russia wakishiriki kwenye sherehe ya kijeshi. Picha ya maktaba.

Uamuzi wa Moscow wiki hii wa kupanua uwezo wake wa kijeshi ni dalili ya changamoto inazopitia Russia, kwenye mwaka wa tatu wa uvamizi wake dhidi ya Ukraine, huku ukionekana kujikokota.

Wachambuzi wanasema kuwa kutokaribishwa kwa hatua hiyo ndani ya nchi, ni kati ya sababu nyingine kumepelekea Russia kutafuta mamluki kutoka mataifa mengine. Septemba 16 rais wa Russia Vladimir Putin alitia saini amri ya kuongeza idadi ya wanajeshi 180,000, ili kufikia jumla ya wanajeshi milioni 2.38, kikiwa kikosi cha pili kwa ukubwa duniani, baada ya China.

Maafisa wa Kremlin wamesema kuwa hatua hiyo ni kwa ajili ya kufanya uvamizi kamili dhidi ya Ukraine, pamoja na kujibu kile Moscow imetaja kuwa “tishio” kutoka kwa NATO, kwenye mpaka wake wa magharibi. Miaka mwili iliyopita, Russia ilifanya uandikishaji mkubwa wa wanajeshi ulioongeza wanajeshi 300,000, kwenye vikosi vyake.

Hata hivyo baadhi ya wachambuzi wanasema kuwa Russia huenda ikalazimika kutumia mbinu tofauti wakati huu. Ripoti za kiuchunguzi kutoka vyombo huru vya habari, vikiwemo The Moscow Times na The Kyiv Independent, zimesema kuwa mawakala wa Russia wanaahidi mishahara mikubwa kwa watu waliofikisha umri wa kuingia vitani, kwenye mataifa kama Sri Lanka, Indonesia, India na Nepal, madai ambayo Kremlin haijakubali wala kukataa.

Ripoti hizo zimesema pia kwamba wale watakaochukuliwa hawatawekwa chini ya vikundi vya mamluki kama lile la Wagner Group, bali watakuwa chini ya jeshi la serikali.