Jumuiya kuu ya uchumi ya mataifa ya Afrika Magharibi ECOWAS imesema ina wasiwasi kuhusu jaribio la mapinduzi na kuwataka waliopanga njama kumuachia huru rais Bazoum.
Jeshi la taifa lilikuwa tayari kuwashambulia walinzi hao endapo hawata jirudi, ilisema taarifa kutoka ofisi ya rais. Taarifa hiyo ilifuatia ripoti kuwa walinzi wa rais wamekata mawasiliano ya kuingia Ikulu na kumzuia rais Bazoum akiwa ndani, kuongeza wasiwasi wa kutokea kwa mapinduzi ya sita katika nchi za Afrika Magharibi tangu 2020.
"Rais wa Jamhuri na familia yake wako salama," ofisi ya rais ilisema kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii bila kutoa maelezo zaidi.
Taarifa hiyo ilifutwa baadaye huku kukiwa na mashaka juu ya nani alikuwa anadhibiti. Wanajeshi walikuwa wamechukua udhibiti wa barabara zote zinazoelekea kwenye kituo cha taifa cha televisheni ambacho kilikuwa kikionyesha sinema.
Maeneo mengine ya mji wa Niamey yalikuwa shwari, magari barabarani yalikuwa kama kawaida na huduma za internet zilikuwa nzuri, mwandishi wa habari wa Reuters amesema.
Chanzo cha habari hii ni shirika la habari la Reuters .