Mwendesha baiskeli wa Misri afutwa kushiriki michezo ya Olimpiki

Picha ya maktaba ya waendesha baiskeli.

Mwanariadha wa kuendesha baiskeli wa Misri Jumapili ameondolewa kwenye orodha ya kushiriki kwenye michezo ya Olimpiki na kamati ya kitaifa ya Olimpiki, baada ya video iliosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kumuonyesha akimgonga mwenzake na kumuangusha kutoka kwa baiskeli yake.

Taifa hilo kubwa zaidi la Kiarabu linajitahidi kuona iwapo litashinda ombi la kuwa mwenyeji wa Olimpiki mwaka wa 2036, na iwapo litafaulu, basi itakuwa ni mara ya kwanza kwa michezo hiyo kufanyikia Afrika. Misri imetumia mabilioni ya dola kutengeneza viwanja vyake, pamoja na kutuma kundi kubwa zaidi kwenye michezo ya Olimpiki ya mwaka huu itakayofanyikia Paris, Ufaransa.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, wakati wa kuwania ubingwa wa kitaifa Aprili, video ya kwenye mitandao, ilionyesha Shahd Saied, akigongana na mmoja wa washindani wenza, Ganna Eliwa, na kisha kumuangusha kabla ya kuendelea na safari yake. Eliwa alimlaumu Saied kwa kumshambulia kwa makusudi, akisema kuwa alishikwa na kiwewe, kando na kujeruhiwa karibu na bega, na kupoteza fahamu kwa muda.

Saied kwa upande wake amejitetea akisema kuwa ilikuwa ni ajali, lakini kamati imempiga marufuku ya kushiriki michezo hiyo kwa muda wa mwaka mmoja.