Mwanariadha aliyechomwa moto na mpenzi wake wa zamani aagwa Kenya

Rebecca Cheptegei kwenye mbo za Marathoni huko Budapest, Hungary - Augosti 26, 2023. Picha na REUTERS/Dylan Martinez/File Photo

Waombolezaji wamekusanyika Eldoret, Kenya siku ya Ijumaa kumuaga mwanariadha wa mbio za Marathon za Olimpiki Rebecca Cheptegei ambaye kifo chake cha kusikitisha kimefufua wito wa kutaka hatua zichukuliwe dhidi ya mauaji ya wanawake katika eneo hilo.

Cheptegei mwenye umri wa miaka 33, alifariki Septemba 5, baada kuchomeka zaidi ya asilimia 75 ya mwili wake katika shambulio linalotuhumiwa kufanywa na mpenzi wake wa zamani, Dickson Ndiema Marangach, tarehe moja Septemba.

Waombolezaji walionekana wakiwa wamebeba jeneza la Cheptegei wakati mama yake Agnes Cheptegei akilia hadharani, akibembelezwa na watu waliomzunguuka.

Mwanariadha huyo, ambaye amemaliza mbio za Olimpiki za Paris alikumbukwa kama mwanga wa matumaini katika jamii ya wakimbiaji ya Kenya.

“Rebeka alistahili kulindwa, Tirop alistahili kulindwa” alisema Marylize Biubwa, mwanaharakati aliyekuwa katika mazishi. Maneno yake yanaashiria Agnes Tirop, mwanariadha mwingine aliyeuawawa mwaka 2021, akiangazia suala la ukatili dhidi ya wanawake katika jumuiya ya wamariadha wa eneo hilo.

Kifo cha Cheptegei kimeongeza wito wa kutaka hatua zichukuliwe juu ya ukatili dhidi ya wanawake nchini Kenya na kwingineko.

Utafiti wa serikali wa mwaka 2022 umeripoti kuwa takribani asilimia 34 ya wanawake wa Kenya wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 49 wamekumbana na ukatili wa kimwili, huku wanawake walioolewa wakiwa hatarini zaidi.