Mshukiwa wa mauaji ya mwanariadha Cheptegei aripotiwa kufariki

Picha ya Rebecca Cheptegei aliyeuwawa na mpenzi wake baada ya kurejea kutoka Olimpiki.

Aliyekuwa mpenzi wa mwanariadha  wa Uganda Rebecca Cheptegei, anayedaiwa kumuuwa kwa kumchoma baada ya kummwagia petroli, ameripotiwa kufariki pia, kutokana na majeraha ya moto aliyopata wakati wa tukio hilo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, taarifa hiyo imetolewa Jumanne, na hospitali moja ya Kenya alipokuwa akipatiwa matibabu. Cheptegei mwenye umri wa miaka 33, aliyeshiriki kwenye michezo ya Olimpiki ya hivi karibuni mjini Paris, alikufa siku nne baada ya shambulizi hilo la Septemba mosi, kutokana na majeraha ya moto ya zaidi ya asilimia 75 kwenye mwili wake.

Mpenzi wake wa zamani Dickson Ndeima Marangach, naye ameripotiwa kufa Jumatatu jioni, kulingana na msemaji wa hospitali ya Rufaa ya Moi Teaching mjini Eldoret, magharibi mwa Kenya, ambapo Cheptegei pia alikuwa akipatiwa matibabu awali kabla ya kufa.

Marangach ameripotiwa kufa kutokana na majeraha ya moto, aliyopata wakati wa shambulizi dhidi ya Cheptegei, alipokuwa akitoka kanisani akiwa na watoto wake. Cheptegei ni mwanariadha wa 3 kuuwawa nchini Kenya tangu Oktoba 2021, na kifo chake kimeangazia mizozo ya nyumbani kwenye taifa hilo la Afrika Mashariki, na zaidi miongoni mwa wanariadha.