Mashambulizi kati ya majeshi ya Afghanistan, Taliban yaingia siku ya nne

Vikosi vya ulinzi vya Afghanistan

Mapambano kati ya wanajeshi Afghanistan na wapiganaji wa Taliban yaliendelea kwa siku ya nne mfululizo leo Jumatatu katika mji wa jimbo la Ghazni, magharibi mwa Kabul, Afghanistan.

Maafisa wanasema wanajeshi zaidi wamepelekwa ili kusaidia kuwarudisha nyuma wapiganaji wa Taliban walioingia ndani kabisa ya mji huo.

Mapigano ya hapa na pale yalizuka Jumapili kati ya wanajeshi wa usalama na wapiganaji wa Taliban kufuatia madai yanayo kinzana iwapo serikali au waasi wa Taliban wanadhibiti vituo muhimu.

Mkuu wa jeshi wa Afghanistan, Jenerali Mohammad Sharif Yaftali aliwaambia waandishi wa habari jana mjini Kabul kwamba wanajeshi wake walifanya mapambano ya kuwaondoa wapiganaji wa Taliban kutoka kwenye mji wa Ghazni.

Jenerali huyo aliongeeza kwamba waasi waliweka kambi ndani ya maeneo ya raia na maeneo ya soko, na kulazimisha wanajeshi wa Afghanistan kusonga mbele kwa uangalifu na taratibu ili kuzuia vifo vya raia.