Maafisa kadhaa wa serikali ya zamani ya Mali wafikishwa mahakamani katika kesi ya ununuzi wa ndege ya rais

Kiongozi wa kijeshi wa Mali, Kanali Assimi Goita katika siku ya mwisho ya kampeni ya kura ya maoni kuhusu katiba mpya, Juni 16, 2023. Picha ya Reuters

Mawaziri kadhaa wa zamani wa Mali na maafisa wakuu wa kijeshi walifikishwa mahakamani Jumanne kujibu tuhuma za kupora mamilioni ya dola wakati wa ununuzi wa ndege ya rais mwaka 2014 pamoja na zana za kijeshi.

Kesi hiyo ni ya muhimu nchini Mali ambapo viongozi wa sasa wa kijeshi walioingia madarakani baada ya mapinduzi ya 2020 ambayo walisema yalikuwa na lengo la kutokomeza ufisadi katika serikali ya rais Ibrahim Boubacar Keita, na kushindwa kwake kupambana na wanajihadi na waasi.

Ndege hiyo ya rais ilinunuliwa dola milioni 40 wakati huo, na kiwango kikubwa cha silaha zilinunuliwa bila soko lolote la zabuni.

Kesi hiyo ilipelekea shirika la kimataifa la fedha (IMF) kuzuia fedha kwa Mali kwa kipindi cha miezi sita.

Waziri mkuu wa zamani Soumeylou Boubeye Maiga, ambaye alikuwa waziri wa ulinzi wakati ununuzi huo ulipofanyika, na waziri wa zamani wa fedha Bouare Fily Sissoko walizuiliwa jela mwaka 2021 kutokana na kesi hiyo.

Walishtumiwa kwa ulaghai, udanganyifu na upendeleo.

Maiga, ambaye aliendelea kusema hana hatia, alifariki gerezani mwezi Machi mwaka jana. Wafuasi wake waliushtumu utawala wa kijeshi kwa kumuacha afiye gerezani.