Kifo cha kwanza charipotiwa katika maandamano ya kupinga kuahirishwa kwa uchaguzi wa rais nchini Senegal

Polisi wa Senegal wakijaribu kuzima maandamano ya kupinga kuahirishwa kwa uchaguzi. Februari 4, 2024. Picha ya Reuters

Polisi wa Senegal waliwafyatulia gesi ya kutoa machozi waandamanaji siku ya Ijumaa huku hasira ikiongezeka juu ya kuahirishwa kwa uchaguzi wa rais. Kifo cha kwanza kimeripotiwa katika maandamano hayo.

Mwanafunzi mmoja aliuawa katika mji wa kaskazini wa Saint Louis, kulingana na marafiki zake, huku maandamano yakienea kote katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Polisi walifyatua gesi ya kutoa machozi kuwazuia waandamanaji waliokuwa wanaelekea mjini kati Dakar, ambako maandamano yalikuwa yamepangwa kufanyika. Mamia ya waandamanaji waliwarushia mawe polisi na kuchoma matairi.

Hasira iliongezeka tangu Rais Macky Sall alipoahirisha uchaguzi wa rais uliopangwa kufanyika Februari 25 hadi Disemba mwaka huu.

Vurugu zilienea katika maeneo mengine ya mji mkuu na kusababisha kufungwa kwa barabara kuu, barabara za reli na masoko makuu.

Maandamano yalifanyika pia katika miji mingine, kulingana na ripoti za mitandao ya kijamii.

Chanzo kwenye hospitali ya mji wa Saint Louis kimelithibitishia shirika la habari la AFP kifo cha mwanafunzi huyo.