Jeshi la Israel lawasilisha waraka wa mpango wa mapigano dhidi ya Gaza

  • VOA News

Wanajeshi wa Israel wakiwa karibu na malori ya kupeleka misaada kwenye Ukanda wa Gaza

Ofisi ya waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu  Jumatatu imesema kuwa jeshi la Israel limewasilisha waraka mbele ya Baraza la Mawaziri la Vita, unaoelezea mpango wa kuwaondoa  raia kutoka kwenye maeneo ya mapigano ndani ya Ukanda wa Gaza, pamoja na mikakati ya operesheni katika siku zijazo.

Taarifa hiyo inafuatia ahadi ya Netanyahu ya kushinikiza mipango ya mashambulizi ya ardhini kwenye mji wa kusini mwa Gaza wa Rafah, ambako zaidi ya nusu ya wakazi wa Gaza wamechukua hifadhi kutokana na mapigano.

Hata hivyo taarifa hiyo haijaeleza kwa kina kuhusu ni wapi wa-Palestina wataweza kwenda. Mji wa Rafah uko kwenye mpaka kati ya Ukanda wa Gaza na Misri, wakati maeneo ya kaskazini mwa Gaza yakiwa yameharibiwa na vita vya miezi minne, Misri imesema haitafungua mipaka yake.

Umoja wa Mataifa umeelezea wasi wasi wake kuhusu mpango wote wa kuwaondoa raia ndani ya Gaza, pamoja na mipango ya Israel wa kuanza kuanzisha mashambulizi kwenye maeneo yenye watu ambao tayari wanahitaji misaada ya kibinadamu.

Katibu mkuu UN Antonio Guterres amesema leo kwamba misaada ya kibinadamu ndani ya Gaza haitoshi kabisa, na kwamba mashambulizi ya Israel huko Rafah huenda yakahujumu sana juhudi hizo.