Japan yatahadharisha kuhusu ushirikiano kati ya Russia na Korea Kaskazini

  • VOA News

Waziri mkuu wa Japan, Fumio Kishida.

Kuongezeka kwa ushirikiano wa kijeshi kati ya Russia na Korea Kaskazini kumepelekea umuhimu wa Japan wa kuimarisha ushirikiano wake na muungano wa NATO,  wakati  tishio la kieneo limekuwa likiongezeka, waziri mkuu wa Japan Fumio Kishida, ameliambia shirika la habari la Reuters.

Kupitia ujumbe wa maandishi kabla ya kuhudhuria mkutano wa NATO mjini Washingtoin DC wiki hii, Kishida pia ameelezea wasi wasi wake kuhusu jukumu la Beijing kuisaidia Russia kwenye vita vyake vya miaka miwili dhidi ya Ukraine, ingawa hakuitaja China moja kwa moja.

“ Usalama wa Euro-Atlantic na Indo Pacific hauwezi kutenganishwa, na uchokozi wa Russia dhidi ya Ukraine, pamoja na kuongezeka kwa ushirikiano wa kijeshi na Korea Kaskazini, ni ukumbusho wa hilo,” amesema Kishida.

Kiongozi huyo amesema kuwa dunia inahitaji kupinga juhudi za baadhi ya mataifa kutaka kuvuruga utaratibu wa kimataifa, akionya kuwa leo ni Ukraine, na kesho inaweza kuwa sehemu nyingine Mashariki mwa Asia.

Korea Kusini, Australia na New Zealand ambao pamoja na Japan wanajulikana kama Indo-Pacific Four (IP4), pia wanahudhuria mkutano wa NATO hapa Washington, Jumatano na Alhamisi.