Israel yaongeza mashambulizi huko Gaza na Lebanon

Mashambulizi ya kuvuka mpaka kati ya Hezbollah na Israel, Septemba 30, 2024. Picha ya Reuters

Israel Jumapili iliongeza mashambulizi yake ya mabomu kaskazini mwa Gaza na kusini mwa Lebanon katika vita vipana dhidi ya makundi ya wanamgambo yanayoungwa mkono na Iran katika kanda hiyo.

Maafisa wa Palestina wamesema shambulizi moja kwenye mskiti liliua watu 19.

Mwaka mmoja baada ya shambulizi la tarehe 7 Oktoba, Israel ilianzisha mapambano mapya huko Lebanon dhidi ya Hezbollah, ambayo ilishambuliana na Israel kwenye mpaka tangu kuanza kwa vita vya Gaza. Mapigano mapya yalianza katika vitongoji vya Beirut Jumapili jioni, video ya AP ilionyesha.

Israel iliapa pia kuishambulia Iran baada ya shambulizi la kombora la masafa marefu dhidi ya Israel wiki iliyopita.

Israel ilikuwa katika tahadhari kubwa kabla ya matukio ya kumbukumbu ya shambulizi la Oktoba 7, huku maandamano yakiendelea ulimwenguni kote kuadhimisha kumbukumbu hiyo.

Shambulizi la kisu na la risasi katika kituo cha basi huko Beersheba lilimua afisa wa polisi wa mpakani, polisi walisema.

Hawakumtambulisha mshambuliaji lakini wamelichukulia kama shambulizi la kigaidi.

Israel imesema inailenga Hezbollah, jeshi lenye nguvu zaidi nchini Lebanon, ambalo limetaja mashambulizi yake ya roketi ndani ya Israel kuwa ishara ya kuwaunga mkono Wapalestina.

Shirika la habari la serikali ya Lebanon limeripoti zaidi ya mashambulizi 30 usiku kucha kuamkia Jumapili.

Jeshi la Israel limethibitisha kuwa lilishambulia malengo ya Hezbollah karibu na Beirut na kusema makombora 130 yalivuka kutoka Lebanon hadi kwenye ardhi ya Israel, huku baadhi yakinaswa.

Shambulizi moja liliua dada watatu na shangazi yao katika kijiji cha pwani cha Jiyyeh.

Wizara ya afya ilisema watu 25 waliuawa katika mashambulizi ya Israel siku ya Jumamosi.