Iran yarusha zaidi ya makombora 150 ndani ya Israel

  • VOA News

Baadhi ya silaha zilizorushwa na Iran zikiwa kwenye anga ya Israel, kabla ya kugonga ardhi Jumanne jioni. Oktoba 1, 2024

Iran Jumanne imefanya shambulizi kubwa la makombora dhidi ya Israel, hatua ambayo inaashiria kusambaa kwa mzozo kati ya Israel na mataifa ya Kiislamu ya kieneo.

Jeshi la Israel limesema kuwa kombora la kwanza kutoka Iran lilirushwa saa moja na nusu jioni kwa saa za huko, na kisha kuendelea kwa takriban nusu saa. Ripoti zimeongeza kusema kuwa Iran ilirusha takriban makombora 180. Chombo cha habari cha serikali ya Iran, IRNA, kilionyesha video ya mashambulizi hayo kupitia ukurasa wake wa Telegram.

Pia taarifa ilitolewa kwamba jeshi la Iran na Revolutionary Guard Corps, IRGC, lilishambulia “ malengo ya kiusalama na kijasusi” ndani ya Israel, kama njia ya kulipiza kisasi kutokana na mauaji ya Julai, ya kiongozi wa Hamas wa Kipalestina, Ismail Haniyeh mjini Tehran, pamoja na mauaji ya karibuni ya makamanda wengine wa Hezbollah nchini Labanon.

Ijumaa iliyopita, Israel iliua kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah kwenye kituo cha kundi hilo kusini mwa Beirut. Brigedia Jenerali wa jeshi la Iran Abbas Nilforoushan pia aliuwawa wakati wa shambulizi hilo. Kufikia sasa, Israel haijakiri wala kukana kuhusika kwenye kifo cha Haniye.

Iran imesema kuwa shambulizi la Jumanne dhidi ya Israel liliidhinishwa na Baraza la Usalama la Kitaifa la Iran, lililopo chini ya ofisi ya kiongozi wa taifa hilo Ayatollah Ali Khamenei.