Hawaii: Rais Biden aahidi kuwasaidia manusura wa janga la moto wa msituni

Rais Joe Biden akiwa na viongozi wa mji wa kihistoria wa Lahaina huko Hawaii.

Rais wa Marekani Joe Biden Jumatatu ameahidi kuwasaidia manusura wa janga la moto wa msituni huko Hawaii kujenga maisha yao tena, takriban wiki mbili baada ya moto huo kuua watu wasiopungua 114 na kuharibu maelfu ya nyumba na kufuta sehemu kubwa ya historia ya mji wa Lahaina.

Biden na mke wake Jill Biden walitembelea kisiwa cha Hawaii cha Maui ambako walikutana na maafisa kadhaa, akiwemo Gavana Josh Green, na kuwashukuru wafanyakazi wa huduma ya kwanza kwa kazi yao kufuatia moto ulioleta balaa.

“Kutokana na taarifa za kuhuzunisha, tumejionea maelezo mengi yenye kutupa moyo na kuonyesha ushujaa, ya itikadi ya aloha. Kila mfanyakazi wa dharura waliyaweka maisha yao hatarini kwa ajili ya kuwaokoa wengine,” Biden alisema. “Mashujaa wa kila siku, majirani wakiwasaidia majirani, viongozi wa asili wa Hawaii wakiwafariji na kuwapa nguvu.”

Rais Joe Biden akiwa na jamii ya waathirika wa janga la moto wa msituni wa Maui katika kituo cha Lahaina Aug. 21, 2023, huko Lahaina, Hawaii.

Biden alisema nchi inaomboleza vifo vya waathirika, na kuwa uongozi wake utafanya kila linalowezekana kusaidia juhudi za kurejesha hali ya kawaida na kuheshimu utamaduni wa eneo wakati ujenzi mpya ukianza.

“Kwa muda wowote utakaochukua, tutakuwa pamoja na nyinyi,” Biden alisema, akiwa amesimama karibu na mti aina ya banyan wenye umri wa miaka 150 huko Lahaina ambao uliteketezwa na moto, lakini bado ulikuwa wima. Alisema kuwa mti huo ulinusurika kwa sababu maalum.”

“Ninaamini ni ishara muhimu sana ya uwezo wetu na kile tunachoweza kufanya katika kuvuka janga hili,” alisema.

Biden alituhumiwa na baadhi ya Warepublikan kwa kutochukua hatua za kutosha mara tu baada ya janga hilo la moto kutokea.

Baadhi ya taarifa katika ripoti hii inatokana na mashirika ya habari ya AP na Reuters.