Hawaii: Idadi ya waliofariki kutokana na moto kwenye kisiwa cha Maui yafikia 80

Moto ulivyoteketeza kisiwa cha Maui, Hawaii.

Idadi ya waliopoteza maish yao kutokana na moto ulioteketeza sehemu za kisiwa cha Maui, katika jimbo la Hawaii, nchini Marekani imepanda hadi 80, maafisa walisema Jumamosi.

Moto huo ndio janga baya zaidi kuwahi kutokea kwenye jimbo la Hawaii tangu kimbunga cha Tsunami kuua watu 61 kwenye Kisiwa hicho Kikubwa mnamo mwaka wa 1960.

Maswali yanaendelea kuulizwa, hata hivyo, kuhusu mifumo ya onyo ya kisiwa kidogo cha Maui, na kutofaulu kwake kuwaonya wakazi kwa wakati.

Meya wa kaunti hiyo Richard Bissen alisema kwenye kipindi cha The Today cha NBC kwamba moto huo ulisambaa haraka sana. Alisema, "Nadhani hii ilikuwa hali isiyowezekana."

Mwanasheria mkuu wa Hawaii, Anne Lopez, alisema afisi yake itatathmini maamuzi yaliyofanywa, na sera zilizopo za Maui kuhusiana na moto wa msituni.

"Idara yangu imejitolea kuelewa maamuzi ambayo yalifanywa kabla na wakati wa moto na kutoa kwa umma matokeo ya ukaguzi huu," alisema katika taarifa Ijumaa.

Mji wa kihistoria wa mapumziko wa karne nyingi wa Lahaina, ulionekana kuteketezwa kwa dakika chache.

Hali ambayo kisiwa hicho kilikuwa kikikabili, huenda ilimkumba kila mtu kutokana na mchanganyiko hatari wa upepo na moto.

Idadi ya waliofariki inatarajiwa kuongezeka zaidi huku timu za utafutaji zikiwa na mbwa, zikiingia kwenye majengo ya kisiwa hicho yaliyochomeka.

Mamlaka imewaonya wakazi wa kisiwa hicho kwamba afueni itachukua miaka na mabilioni ya dola.