Benki ya dunia inasema Denmark imeahidi dola milioni 491 kwa nchi maskini

Nembo ya Benki ya dunia

Benki ya dunia Jumatatu ilisema kwamba Denmark imeahidi kutoa mchango wa dola milioni 491.7 kwa mfuko wa benki hiyo ili kusaidia nchi maskini, likiwa ongezeko la asilimia 40 ikilinganishwa na mchango wa awali wa nchi hiyo.

Benki ya dunia imesema ina lengo la kuchangisha rekodi ya fedha kwa mfuko wake wa maendeleo ya kimataifa (IDA) ifikapo mwezi Disemba, kupiku michango ya awali ya dola milioni 93 mwezi Disemba 2021.

Lakini kampeni ya kukusanya zaidi ya dola bilioni 100 inajiri wakati wa rasimali ndogo za kifedha, huku nchi nyingi tajiri zikipunguza matumizi, kutokana na kususua kwa uchumi wao baada ya janga la Covid 19.

Ahadi hiyo ya dola milioni 491.7 ambayo Denmark iliitangaza kwenye mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, ni ahadi kubwa kwenye sekta ya maendeleo, wakati mahitaji ya ufadhili yanazidi kuongezeka kwa nchi zenye kipato cha chini zinazokabiliwa na madeni.