Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumapili, Septemba 08, 2024 Local time: 20:30

Wanaharakati nchini Sudan wanasema RSF wameua watu 65 katika mji wa El-Fasher


Picha hii iliyochapishwa kwenye mtandao wa X wa kundi la RSF Julai 28, 2023, inamuonyesha kamanda wa RSF, Mohamed Hamdan Dagalo.
Picha hii iliyochapishwa kwenye mtandao wa X wa kundi la RSF Julai 28, 2023, inamuonyesha kamanda wa RSF, Mohamed Hamdan Dagalo.

Takriban watu 65, wengi wao wakiwa watoto waliuawa tangu siku ya Jumamosi katika mashambulizi ya mabomu yaliyofanywa na wanamgambo wa kikosi cha Rapid Support Forces (RSF) katika mji wa jimbo la Darfur wa El-Fasher, wanaharakati wamesema.

Mji huo wa jimbo la Darfur Kaskazini ndio mji mkubwa ambao haujadhibitiwa na kundi la RSF, ambao limeuzingira tangu mwezi Mei.

Vita kati ya RSF na jeshi la Sudan vimepamba moto tangu vilipozuka mwezi Aprili mwaka jana.

The El-Fasher Resistance Committee Jumatatu walisema katika taarifa kwamba “ katika kipindi cha siku tatu RSF waliua zaidi ya watoto 43, wanawake 13 na wanaume tisa miongoni mwa wakazi wa El Fasher”.

“Leo ni moja ya siku za mauaji mabaya mjini El-Fasher, dhidi ya raia, misikiti, hospitali, hasa hospitali ya Saudi”, gavana wa jimbo la Darfur Mini Minawi aliandika kwenye mtandao wa X.

Chanzo cha matibabu katika hospitali ya Saudi, ambayo ilishambuliwa vikali, awali kilisema shambulizi la mizinga liliua watu 22 Jumamosi.

Minawi aliongeza kuwa RSF walipokea “siku mbili zilizopita mfumo wa makombora kutoka El-Geneina”, mji mkuu wa Darfur Magharibi.

Vita vya Sudan kati ya kikosi cha RSF kinachoongozwa na Mohamed Hamdan Dagalo na jeshi la Sudan linaloongozwa na Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, vimeua maelfu ya watu, huku baadhi ya makadirio yakisema watu 150,000 wameuawa, kulingana na mjumbe wa Marekani kwa ajili ya Sudan Tom Perriello.

Forum

XS
SM
MD
LG