Marekani imekuwa mfadhili mkubwa wa kikosi hicho kinachoongozwa na polisi wa Kenya, ambacho kilianza shughuli zake mwaka jana na kinakabiliwa na ukosefu wa fedha na wafanyakazi.
Kusitishwa kwa ufadhili huo kutakuwa na “athari za moja kwa moja” kwa kikosi hicho, msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric alisema.
Hatua hiyo inajiri baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutoa amri ya kuzuia misaada ya kigeni, na kusababisha maelfu ya wafanyakazi na wanakandarasi wa Idara ya Marekani ya maendeleo ya kimataifa (USAID) kuachishwa kazi na program nyingi za idara hiyo kusitishwa ulimwenguni kote.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio aliruhusu program za kuokoa maisha ziendelee, lakini bado kuna mkanganyiko kuhusu kipi kinaruhusiwa kutolewa katika amri ya kiutendaji ya rais na hofu ya kukosa misaada ya Marekani kabisa, inakwamisha utoaji wa misaada na kazi ya maendeleo duniani kote.
Marekani ilikuwa imeahidi kutoa dola milioni 15 kwa mfuko wa Umoja wa Mataifa unaosaidia kufadhili kikosi cha Kimataifa nchini Haiti, Dujarric alisema.
Dola milioni 1.7 zimekwisha tumiwa, “dola milioni 13.3 sasa zimezuiliwa,” Dujarric aliongeza.
Mfuko huo wa Umoja wa Mataifa unasalia na chini ya dola milioni kwa jumla ya dola milioni 600 zinazohitajika kila mwaka kwa kikosi hicho cha kimataifa.
Maafisa wanaoongoza kikosi cha Kenya hawakutarajia usitishwaji wa ufadhili huo. Msemaji wa kikosi hicho Jack Mbaka hakutoa maelezo ya mara moja kwa shirika la habari la AP.
Forum