Zimbabwe yadai vikwazo vyaisababishia kupoteza zaidi ya dola bilioni 150

Rais wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa (kulia) akiwa na makamu wa rais Constantino Chiwenga (kushoto) wakati wa hafla ya kuwaapisha mawaziri wapya wa Baraza la Mawaziri huko Harare Septemba 10, 2018. Picha na Jekesai NJIKIZANA / AFP.

Makamu wa rais wa Zimbabwe Jumatano alisema nchi hiyo imepoteza zaidi ya dola bilioni 150 kutokana na vikwazo vilivyowekwa na Umoja wa Ulaya na nchi kama vile Marekani kufuatia ripoti za wizi wa kura na ukiukwaji wa haki za binadamu mwanzoni mwa miaka ya 2000.

Akizungumza na waandamanaji wanaopinga vikwazo hivyo, makamu wa rais Constantino Chiwenga alisema hatua hizo pia zinaumiza kanda yote ya kusini mwa Afrika.

Aliviita vikwazo hivyo kuwa ni "pingamizi kubwa" kwa Zimbabwe, kwa kuwa vinajumuisha vikwazo vya kifedha ambavyo vinaifanya Zimbabwe itengwe katika upatikanaji wa mitaji duniani.

Stevenson Dhlamini, profesa wa uchumi katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Sayansi na Teknolojia nchini Zimbabwe, alisema kiasi cha dola bilioni 150 kinalingana na kile ambacho serikali ya Zimbabwe imekuwa ikikitaja kwa miaka mingi

"malimbikizo ya madhara ya vikwazo vya Marekani, EU na U.K. vina matokeo ambayo yanaweza kufikia kiwango hicho," alisema Dhlamini.

Siyo kila mtu anakubali.

Prosper Chitambara, mchumi mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Maendeleo ya Kazi na Maendeleo ya Uchumi ya Zimbabwe, alisema mambo mengi yameathiri uchumi wa nchi hiyo, siyo tu vikwazo.

Baada ya maandamano hayo ambayo yaliwavutia wengi hasa watumishi wa umma na wafuasi wa chama tawala cha Zanu PF, Chiwenga aliapa kuwa uchumi wa Zimbabwe utashinda dhidi ya vikwazo hivyo.

"Lakini tunakuja na mawazo mengine kabisa," alisema. "Kwa hivyo, vikwazo viwepo au visiwepo, Zimbabwe itafanikiwa."