Waziri mkuu wa Russia kutembelea rais mpya wa Iran mjini Tehran

  • VOA News

Waziri Mkuu wa Russia, Mikhail Mishustin akiongoza mkutano wa baraza la mawaziri mjini Moscow. Mei 15, 2024. (Grigory Sysoyev/Sputnik via Reuters)

Russia imetangaza Jumapili kwamba waziri wake mkuu Mikhail Mishustin, atakutana na rais wa Iran Masoud Pezeshkian mjini Tehran Jumatatu.

Tangazo hilo limekuja wakati Russia ikiilani Israel kwa “ mauaji ya kisiasa” ya kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah mjini Beirut. Mishustin atakuwa na mazungumzo na Pezeshkian, na makamu wa kwanza wa rais Mohammad Reza Aref, taarifa ya serikali imesema. Mkutano wao unatarajiwa kujadili ushirikiano wa Russia na Iran katika biashara biashara na uchumi na utamaduni na masuala ya kibinadamu.

Mataifa ya Magharibi yanaishutumu Iran kwa kuipatia Moscow silaha pamoja na droni kwenye vita vyake na Ukraine, suala ambalo Tehran imelikanusha. Pezeshkian pia amepangiwa kufanya mazungumzo na rais wa Russia Vladimir Putin, wakati wa ziara yake ya Russia mwezi ujao kwenye mkutano wa BRICS.

Baada ya kuondoka Iran, waziri mkuu wa Russia, Mishustin atahudhuria mkutano wa uchumi wa Eurasia, Jumanne nchini Armenia. Russia mara nyingi huiona Umoja wa Kuichumi wa Eurasia, EEU, kama mbadala wa makundi ya kisiasa na kiuchumi ya Magharibi.