Watu wawili wameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa leo Jumanne nchini Bangladesh katika mapambano kati ya polisi na waandamanaji wanaoipinga serikali, siku ya kwanza ya maandamano ya siku tatu ya kumshinikiza waziri mkuu Sheikh Hasina kujiuzulu.
Chama kikuu cha upinzani, Bangladesh National Party (BNP) kimeomba barabara zifungwe kwa siku tatu kufuatia mapambano ya siku ya Jumapili kati ya wafuasi wake na polisi ambapo afisa mmoja wa polisi aliuawa na zaidi ya watu 100 kujeruhiwa.
Chama hicho kimemuomba waziri mkuu Sheikh Hasina ajiuzulu ili kuruhusu uchaguzi uliopangwa mwezi Januari ufanyike chini ya serikali ya mpito isiyoegemea upande wowote. Lakini serikali ya waziri mkuu ilipinga ombi hilo.