Visiwa vya Chagos vyapewa uhuru wa kujitawala na Uingereza

  • VOA News

Ndege ya kijeshi ya Marekani aina ya B-1B bomber, zikiondoka kwenye kituo cha kijeshi cha Diego Garcia, Chagos, kuelekea Afghanistan October 07, 2001.

Uingereza Alhamisi imekubali kuvipatia uhuru wa kujitawala visiwa vya Chagos ambavyo ni zaidi ya 60 vikiwa kwenye Bahari Hindi kwa serikali ya Mauritius, baada ya kuzozaniwa kwa muda mrefu, ikiwa hatua ya kulinda vituo muhimu vya majeshi ya Uingereza na Marekani.

Waziri wa mambo ya Kigeni wa Uingereza David Lammy amesema kuwa makubaliano hayo yatahakikisha usalama wa kituo cha kijeshi cha Diego Garcia, ambacho ni kikubwa zaidi miongoni mwa visiwa hivyo ambavyo vimekuwa himaya ya Uingereza kwa zaidi ya miaka 50.

Kituo hicho chenye takriban wanajeshi 2,500, wengi wakiwa wamarekani kimehusika kwenye operesheni za kijeshi hapo nyuma vikiwemo vita vya Iraq vya 2003 na vile vya Afghanistan vilivyomalizika hivi karibuni. Uingereza imesema kuwa bila kuwa na makubaliano hayo, operesheni za kijeshi huenda zikawa hatarini katika siku zijazo kutokana na mzozo wa kisheria kupitia mahakama za kimataifa pamoja na majopo kadhaa.

Mkataba huo pia inafungua njia ya kurejeshwa kwa watu wachache waliobaki hai, baada ya kuondolewa makwao visiwani humo, miongo kadhaa iliopita. Takriban wakazi 1,500 kutoka visiwa vya Chagos, waliondolewa mwakao ili kutoa nafasi ya kujengwa kwa kituo cha kijeshi cha Marekani, hatua ambayo ilitajwa na kundi la Human Rights Watch kuwa ni uhalifu wa kibinadamu uliotekelezwa na utawala wa kikoloni dhidi ya wenyeji.