Viongozi wa nchi za Afrika wawasili Ukraine katika juhudi za kusuluhisha mzozo kati ya nchi hiyo na Russia

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, waziri mkuu wa Misri Mustafa Madbuly, Rais wa Comoros Azali Assoumani, Rais wa Senegal Macky Sall na Rais wa Zambia Hakainde Hichilema, wahudhuria hafla ya kumbukumbu ya mauaji katika kijiji cha Bucha, nchini Ukraine, Juni 16, 2023.

Ving’ora vya ulinzi wa anga vimesikika Ijumaa katika mji mkuu wa Ukraine, Kyiv wakati ujumbe wa wakuu wa nchi za Afrika wakikutana na viongozi wa serikali ya Ukraine kwa juhudi za upatanishi na matumaini ya kuanzisha mazungumzo ya amani kati ya Ukraine na Russia.

Meya wa Kyiv Vitali Klitschko aliandika kwenye mitandao ya kijamii kwamba kulitokea mlipuko katika wilaya ya kati ya Podil.

Baadaye Klitschko alisema kwamba milipuko iliyosikika mjini Kyiv ilisababishwa na mifumo ya ulinzi wa anga karibu na mji mkuu.

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ni miongoni mwa ujumbe huo wa Umoja wa Afrika ambao unakutana na Rais wa Ukraine Volodymr Zelenskiy, hatua ya kwanza katika jukumu la kutafuta makubaliano ya amani kati ya Kyiv na Moscow.

Wajumbe wengine ni Rais wa Senegal Macky Sall, Rais wa Zambia Hakainde Hichilema na Rais wa Comoros Azali Assoumani, ambaye ndiye mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika.

Marais wengine watatu, wa Jamhuri ya Congo, Misri na Uganda walitarajiwa kushiriki katika ujumbe huo lakini badale yake walituma wawakilishi.

Baada ya kukutana na Rais Zelenskiy leo Ijumaa, marais hao watasafiri kuelekea Russia kukutana na Rais Vladimir Putin.