Viongozi wa Afrika wameomba Russia iruhusiwe tena kuuza nje nafaka yake

Wajumbe kwenye mkutano kati ya Russia na viongozi wa Afrika mjini Saint Petersburg, Julai 28, 2023.

Viongozi wa Afrika wanaohusika katika mazungumzo ya amani kuhusu Ukraine wametoa wito wa kuanzishwa tena mauzo ya nafaka na mbolea ya Russia ili kufufua makubaliano muhimu ya nafaka ya Ukraine ya Bahari ya Black Sea, Afrika Kusini ilisema Alhamisi.

Kundi hilo la viongozi wa Afrika lilitoa pia wito kwa Umoja wa Mataifa kuchukua hatua ili kuachilia tani 200,000 za mbolea ya Russia zinazozuiliwa katika bandari za bahari za Umoja wa Ulaya, alisema Vincent Magwenya, msemaji wa Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa.

“Viongozi hao wameomba hatua mahususi zichukuliwe ili kuondoa vikwazo kwa mauzo ya nafaka na mbolea ya Russia, na hivyo kuruhusu kuanzishwa tena kwa mpango kamili wa bahari ya Black Sea,” Magwenya aliuambia mkutano wa waandishi wa habari mjini Pretoria.

Russia mwezi uliopita iliondoka kwenye makubaliano yaliyosimamiwa na Umoja wa Mataifa na Uturuki ambayo yaliruhusu mauzo ya nafaka ya Ukraine kupitia bandari ya Black Sea, na kusababisha kupanda kwa bei ya nafaka, hali ambayo iliziathiri vibaya nchi maskini.

Russia inaomba uhakikisho kwenye makubaliano mengine yanayohusu mauzo yake ya nje, hasa ya vipengele vya mbolea.

Wito huo ili kukidhi baadhi ya maombi ya Kremlin ulitolewa na Ramaphosa na marais wengine sita, wakiwemo Abdel Fattah al-Sisi wa Misri na Macky Sall wa Senegal, baada ya mazungumzo na Putin mjini St Petersburg wiki iliyopita, Magwenya alisema.