Vijana 70 bado hawajulikani walipo kufuatia ajali ya shule ya bweni Kenya

Wazazi wakiwa nje ya jengo la shule ya bweni ya Hillside Endarasha Academy huko Nyeri. September 6, 2024.

Watoto 17 wenye umri kati ya miaka tisa na 13 wamepoteza maisha na wengine wamepata majeraha wapo hospitalini.

Familia za watoto katika shule ya msingi ya bweni nchini Kenya ambako moto ulisababisha vifo vya wavulana 17 zilikabiliwa na hali ya taharuki leo Jumamosi wakisubiri taarifa za wapendwa wao waliopotea.

Naibu Rais wa Kenya Rigathi Gachagua, aliwaambia waandishi wa habari katika eneo la tukio siku ya Ijumaa kwamba vijana 70 bado hawajulikani waliko.

Moto katika shule ya Hillside Endarasha Academy iliyopo katika kaunti ya kati ya Nyeri ulizuka Alhamisi usiku, na kuteketeza bweni moja ambako zaidi ya wavulana 150 walikuwa wamelala.

Rais William Ruto ametangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa kuanzia Jumatatu baada ya kile alichokitaja kuwa “janga lisiloeleweka”. Alisema watoto 17 wenye umri kati ya miaka tisa na 13 wamepoteza maisha yao, huku 14 wakipata majeraha na wanaendelea kupatiwa matibabu hospitali.