Ujumbe wa wapatanishi kutoka nchi za Afrika wawasili Russia kujaribu kumaliza mzozo wa Ukraine

Rais Vladimir Putin wa Rashia akutana na ujumbe wa viongozi wa nchi za Afrika mjini Saint Petersburg, Rashia.

Ujumbe wa wapatanishi kutoka nchi za Afrika unaojaribu kumaliza mzozo wa Russia na Ukraine unaoongozwa na Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa umewasili Russia siku ya Jumamosi, baada ya kuitembelea Kyiv hapo jana.

Ofisi ya Rais wa Afrika Kusini ilisema kwenye ujumbe wa Twitter kwamba “Rais Ramaphosa na ujumbe wake waliwasili mjini Saint Petersbourg,” kaskazini magharibi mwa Russia ambako alikutana kwanza pekee yake na Rais wa Russia Vladimir Putin, kabla ya mkutano wa pamoja na wapatanishi wote kutoka Afrika,.

Ujumbe huo uliwasili Saint Petersbourg baada ya mazungumzo yenye tija na rais wa Ukraine Volodymry Zelenskyy Ijumaa mjini Kyiv, kulingana na taarifa iliyotangazwa baadaye na ofisi ya Rais wa Afrika Kusini.

Akiwa pamoja na marais wa Zambia, Comoros na Senegal, pamoja na wawakilishi wa Jamhuri ya Congo, Misri na Uganda, Ramaphosa anakutana na Putin ili kutafuta suluhisho la amani baada ya miezi 16 ya mzozo kati ya Russia na Ukraine ambao ulisababisha msukosuko duniani, ofisi ya rais wa Afrika Kusini imesema.