Rais mpya wa Sri Lanka alivunja bunge na kumteua waziri mkuu mwanamke

Rais mpya wa Sri Lanka Anura Kumara Dissanayake wakati wa hafla ya kuapishwa, Septemba 23, 2024.

Rais mpya wa Sri Lanka Anura Kumara Dissanayake alilivunja bunge Jumanne na kuitisha uchaguzi wa bunge ndani ya chini ya wiki tatu katika juhudi za kuimarisha mamlaka yake baada ya ushindi wake kwenye uchaguzi wa mwishoni mwa Juma.

Taarifa hiyo ya serikali ilisema kwamba Bunge limevunjwa kuanzia Jumanne usiku wa manane, na kwamba uchaguzi wa bunge umepangwa kufanyika Novemba 14.

Hatua hiyo ilitarajiwa, kwani Dissanayake aliapa kufanya hivyo wakati wa kampeni yake ya uchaguzi.

Chama cha Dissanayake kina viti vitatu pekee katika bunge lenye wabunge 225 na uchaguzi wa mapema utamsaidia kudhibiti baraza hilo, huku alama za utendaji kazi wake zikiendelea kuwa imara kufuatia ushindi wake katika uchaguzi wa Jumamosi.

Bunge limevunjwa saa chache baada ya Dissanayake kumwapisha mbunge mwanamke kutoka muungano wake kama waziri wake mkuu, na kumfanya kuwa waziri mkuu wa kwanza mwanamke kuiongoza serikali katika kipindi cha miaka 24.

Harini Amarasuriya, mwenye umri wa miaka 54, muhadhiri wa chuo kikuu na mwanaharakati, wote ni kutoka muungano wa vyama vya siasa za Kimarxist, National People’s Coalition, ambao unaendelea kuwa kwenye kambi ya upinzani bungeni.